Wednesday, September 14, 2011

MV SPICE ISLANDERS ILISAFIRI HADI KUZIMU MITHILI YA MV BUKOBA!

AJALI YA MV. SPICE ISLANDERS HAINA TOFAUTI NA YA MV BUKOBA

 
 Tanzania ilikuwa tayari imepitisha  miaka 15  ya kuzama kwa Meli ya Mv.Bukoba pale Mv. Spice Islanders ya Zanzibar ilipozama Bahari ya Hindi.
 Mv. Spice Islander, ilizama Septemba 10,ikifanya safari zake kati ya Unguja na Pemba na kupoteza maisha ya watu zaidi ya 200.
Watu 260 waliokolewa.
 Hadithi ni zile zile za Mv Bukoba, kwamba meli ilipakia watu wengi na mizigo kupita uwezo wake, kwamba abiria wengine walichelea kuipanda; ndivyo ilivyotokea kwa MV Bukoba huko Kemondo Bay.
   Meli ya  Mv. Bukoba,ilizama alfajiri, Mei 21, mwaka 1996 na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 800.
Ilikuwa ikitokea Bukoba, na ilizama kilomita kama 12 za majini kutoka bandari ya Mwanza, uelekeo wa Bwiru, jijini Mwanza.
     Inakisiwa kwamba, watu waliojeruhiwa katika ajali hiyo ya kihistoria ni 100; wakati mali nyingi zilipotea na thamani yake bado kujulikana.
 Mara baada ya ajali ile, serikali iliunda Tume iliyokuwa chini ya Jaji Robert Kissanga, ili kuchunguza chanzo cha ajali ile mbaya ya majini.
  Kulingana na Ripoti ya Tume hiyo, usiku wa kuamkia siku ya ajali(Mei 20 mwaka 1996),meli hiyo ilikuwa na abiria kati ya 750 na 800 na wafanyakazi 37.
Kati hao, 114 waliokolewa, na maiti 391 ndiyo walioopolewa na kuzikwa katika makaburi ya Igoma,jijini Mwanza, wakati miili mingine ilichukuliwa na ndugu zao kwenda kuzikwa.
   Kila mwaka, serikali na wananchi huwasha mishumaa na kufukiza ubani katika makaburi hayo kama kumbukumbu ya ajali ile.
  Pengine, serikali huongozana na watu wa madhehebu ya dini kwenda eneo la ajali ili kusoma dua na kumwaga mchanga majini kama ishara ya ibada ya wafu na maziko.
 Inakisiwa, jumla ya miili 332 haikupatikana.
Kwahiyo, serikali ilifanya ‘mazishi’ ziwani katika eneo la ajali,umbali wa kama maili za majini nane tu kutoka ilipo Bandari ya Mwanza.
    Mv.Bukoba, ilijengwa na kampuni ya Meli ya Kibelgiji.Wakati wa kuzinduliwa,Julai 27 mwaka 1979 ilibainika ilitaka kumtosa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere.
 Haikuwa na uwiano wa majini.
 Ilisemwa kwamba, serikali ilishaipiga marufuku meli hiyo isifanye huduma Ziwa Victoria ,  sababu haikuwa na 'sea worthness', vinginevyo lilikuwa kaburi lenye kuelea, ambali siku na saa yoyote ingesababisha maada makubwa.
  Hata hivyo, kufuatia uzembe wa serikali ama kutojali, Mv. Bukoba iliendelea kukata mawimbi ya Ziwa kutoka Mwanza hadi Bukoba, kila siku hadi ilipozama.Iliazama miaka 15 baadaye.
   Baada ya Tume ya Jaji Robert Kissanga kuwasilisha Ripoti ya uchunguzi wake, serikali ikafungua kesi Mahakama Kuu na kuwashitaki aliyekuwa Nahodha wa Meli, Jumanne Rume-Mwiru, aliyekuwa Mkaguzi wa Mamlaka ya Bandari(THA),Gilbert Mokiwa, Meneja wa Bandari ya Bukoba, Alphonce Sambo, na aliyekuwa Meneja wa Bandari ya Kemondo, Prosper Lugumila.
    Kesi hiyo nambari 22,ilifunguliwa Mahakama Kuu,Mwanza mwaka 1998, na ilianza kusikilizwa Mei 14 mwaka 2001.
   Upande wa Mashitaka ukiongozwa na mawakili wa serikali, William Magoma na Eliezer Feleshi(sasa DPP) ulidai mahakamani hapo kwamba washitakiwa kwa pamoja walisababisha vifo,kujeruhi na upotevu wa mali nyingi(hazikufahamika), kwa uzembe.
   Kesi hiyo ilitajwa mara nyingi, ikaahirishwa zaidi ya mara sita hivi, baada ya kusikilizwa kwa mwaka mzima,tangu ilipoanza kusikilzwa Mei,2001.
   Ijumaa, Novemba 29, mwaka 2002, majira ya saa sita mchana, aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Juxton ,Mlay, akasoma hukumu ya kesi hiyo.Nilikuwepo mahakani wakati hukumu ikisomwa.
  Aliwaachia huru washitakiwa wote wanne, baada ya upande wa mashitaka kushindwa kuithibitishia mahakama(pasipo shaka yoyote) kwamba walisababisha ajali ile na vifo vya watu kama nilivyokwisha taja.
   Jaji Malay, alisema mahakamani wakati akisoma hukumu hiyo ya kihistoria, kwamba hoja za upande wa mashitaka kwamba washitakiwa, Jumanne Mwiru, Mokiwa, Sambo,na Prosper Lugumila walisababisha vifo,kujeruhi na upotevu wa mali, hazikuwa na ushahidi.
   Kwamba, kwa kuwa mashahidi waliiambia mahakama kuwa Rume-Mwiru alisikika asubuhi ile ya ajali, akimwamuru rubani kukata kona, maana yake ni kwamba alikuwa na nia thabiti ya kuokoa maisha ya abiria na wafanyakazi wa meli yake, na wala siyo kutaka kuwaua kwa uzembe kama ilivyodaiwa.
    Akisoma hukumu ndefu, iliyokuwa na jumla ya kurasa 118 zilizvyoandikwa kwa mkono, Jaji Mlay alitumia zaidi ya dakika 160 kufafanua vipengele vya kisheria na kuvitolea maamuzi kwa ufasaha.
   Mwishoni mwa hukumu, akasema kwamba hapakuwa na ushahidi kwamba Mv Bukoba ilizama kwa uzembe wa washitakiwa wanne: Sambo, Mwiru, Mokiwa na Lugumila peke yao !
   Madai ya upande wa mashitaka kwamba Mv.Bukoba ilipakia mizigo mingi kushinda uwezo wake yakatupiliwa mbali na mahakama.
 Kwa sababu, haikufahamika kwa yakini, kwamba MV.Bukoba ilikuwa na abiria wangapi siku ya ajali. Na ilibeba mizigo ya uzito wa kiasi gani?
 Mashahidi wa upande wa mashitaka,walikuwa wameiambia mahakama hiyo kwamba, meli ilipakia mikungu mingi ya ndizi: Lakini, kiasi gani yenye uzito gani?
Nani aliipima uzito?
    Mahakama ilihoji bila majibu. Jaji Mlay alisema, MV.Bukoba ilizama Mei 21, mwaka 1996 kwa sababu haikuwa thabiti; na haikuwa na uwiano wa majini. Hata Tume ya Jaji Kissanga ilisema hivyo.
  Kama kawaida,upande wa mashitaka ukiongozwa Eliezer Feleshi, ukaonesha nia ya kuomba rufaa mahakama ya rufaa.
   Nilikuwepo mahakamani, wakati wa kusomwa hukumu ile.
Niliwaona washitakiwa wakiganda kwa butwaa, kama waliomwagiwa barafu; hawakuamini.
 Nilitaka Jumanne Rume-Mwiru aniambie, alijiskiaje? Hakujibu.
   Miezi mingi baadaye, tulipokutana katika mitaa ya jiji la Mwanza, Mwiru aliniambia kwamba mshitakiwa mwenzake ambaye siku hiyo hakuwepo mahakamani, alipoambiwa kuhusu hukumu ile aliugua nakulazwa hospitalini, mjini Bukoba.
  Leo, ni  miaka mingi  tangu hukumu ile isomwe,rufaa haijasikilizwa, na baadhi ya washitakiwa wamefariki dunia, bila kuona hatma ya kesi yao .
  Mawakili wa upande wa utetezi walikuwa Salum Magongo na Gallati Mwantembe wa jijini Mwanza.
 Mv.Bukoba ilizama kwa sababu za uzembe wa serikali na vyombo vyake.
Haikuwa na uwiano wa majini muda mrefu, hata haikuwa na zana za uokozi kama maboya ya kutosha.
   Haikuwa na mawasiliano.
  Niliwahi kufanya mahojiano na aliyekuwa Nahodha, Jumanne Rume-Mwiru, na kumuuliza hatma ya kesi ile huko mahakama ya rufaa, na kama walikuwa na nia ya kudai mafao yao ?
 “Tunamwachia Mungu” alisema Mwiru huku akicheka bila shaka kukumbuka kilichomtokea.
Aliniahakikishia kwamba mwezao mmoja alikuwa amefariki,bila kujua hatma ya kesi ile.
 Rume-Mwiru, tayari ni marehemu, wakati hatma ya kesi yao haijulikani hadi leo.
   Hata baada ya ajali ile, zimetokea ajali nyingi Ziwa Victoria , mitoni na baharini.
 Mv.Nyamageni,iliyokuwa meli ya binafsi, ilizama miaka ya karibuni ikiwa imebeba masanduku ya soda na abiria kwa pamoja, na haikupatikana hata leo.
 Ilikuwa safari ya kwenda kuzimu.
  Naam, safari ya kuzimu!
Meli za Tanzania ni majeneza yanayosafiri kwenda kuzimu.
Uzembe! Hata ajali za magari huletwa na uzembe tu, usalama barabarani wapo, hakuna hatua. Ziwa Victoria ndipo kuna kazi, majahazi hayana hata boya moja,hakuna vifaa vya kuzima moto!
 miaka ya karibuni, Meli nyingine ya Shirika la Meli(Marine Services Company), Mv.Butiama, ilizimika majini, ikaelea kwa zaidi ya saa nne.
 Meli hiyo ati haikuwa na mawasiliano.
Mtu mmoja alikiambia kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC) Mkoani Mwanza,kuwa ingeweza kupigwa mawimbi hadi Uganda , au ikaparamia mwamba?
   Majibu hayakutolewa, aliyekuwa akiulizwa alikuwa mtaalam kutoka Mamlaka ya Bandari(TPA), kwamba asingeweza kuisemea MSC, ambao hawakualikwa katika mkutano huo.
  Abiria walihaha, Mv.Butiama ilipozima injini zake jirani tu na Bandari ya Mwanza, lakini hakukuwa na mawasiliano. Eti meli za MSC bado hazina maboya na mawasiliano!
 Je, zile za wajasiliamali zinazotia nanga katika bandari zinazomea kama uyoga, zina zana za uokozi?
Zina maboya mangapi na hufuata sheria kwa kiwango gani?
 Bila shaka, zinafanya kazi kwa mazoea kama ilivyokuwa mwaka 47!
Naam, meli za nchi hii, hata leo hii miaka 15 baada ya kuzama kwa Mv.Bukoba ni majeneza yanayosafiri majini
.Hata MV Spice ilikuwa jeneza lililoelea majini, abiria wakapanda,wakasafiri hadi kuzimu! Nawapa pole walionusurika!
  SUMATRA na vyombo vingine vya serikali wapo, wanatazama majahazi yakisafiri ama kuelea kwenda kuzimu.
Serikali huishia kufanya matambiko majini kila mwaka, kama ilivyofanya juzi.
Wengine wamekula ubani wa wafiwa, wengine hujitajirisha kwa maadhimisho haya, wapo tu.
   Wanabarizi upepo.Kufaa kufaana, sijui?
 0754-324 074,0786 324 074
 
 
 
  
  

Top of Form

Thursday, September 1, 2011

BURIANI MUAMMAR AL GADDAFI




SUDAN ya Kusini, sasa ni nchi huru chini ya Rais Salva Kiir; naam ni nchi ya 54 katika Umoja wa Afrika, AU.
 ni sasa ni nchi ya 193 katika Umoja wa Mataifa(UN) uliogeuka Umoja wa Mataifa wa Marekani!

Kanali  Dk. John Garang de Mabior.
Alisafiri hadi kuzimu kwa njia ya helkopta iitwayo, M-72; ambayo awali ilitarajiwa kuruka kutoka jijini Kampala hadi Juba, Kusini mwa Sudan .
   Ilikuwa Julai 30 mwaka 2005; miaka sita  imepita  tangu   kifo chake;kifo kibaya cha ajali ya helkopta iliyopokonya tonge mdomoni.
   D.k John Garang, alikuwa akijiandaa kuwa Makamu Rais wa Sudan kufuatia Mkataba wa amani baada ya kumalizika mapigano dhidi ya serikali ya Khartoum , ya Rais Omar Hassan El-Bashir.
   Kiongozi wa Sudan People’s Liberation Army\Movement (SPLA/SPLM)alikufa katika ajali hiyo ya helkopta ya Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda ; pamoja na maofisa wake wapatao 13 mahali ambapo ni mpakani mwa Uganda na Sudan.Sababu ya ajali hiyo ilisemwa ilitokana na hali mbaya ya hewa.
  Dk. Garang, alikuwa akirejea nyumbani baada ya Mkutano na Rais Yoweri Museveni  mjini Kampala .
Agosti Mosi mwaka huo wa 2005 Salva Kiir, alirithi heshima na harakati za De Mabior za kusaka uhuru Kusini mwa Sudan , taifa la Waarabu wa Kaskazini na Weusi wakulima wa Kusini.
  Sasa, Salva Kiir ni rais wa Sudan ya Kusini iliyopata uhuru punde,kutoka kwa mabedui wa Kiarabu wa Kaskazini.
    Hayati De Mabior alianza harakati za kutafuta uhuru wa watu wake siku nyingi. Kama kawaida ya makamaradi wenzake wote, alilelewa Dar es salaam , ambako ni kitovu cha vuguvugu la uhuru hapa Barani.
   Mashujaa wengine waliowahi ‘kupikwa’ na kuiva kimapinduzi Dar es salaam ni pamoja na  hayati Samora Moises Machel wa Musumbiji, Laurent Desire Kabila wa Jamhuri ya Kongo(DRC), Rais wa sasa wa Kongo, Joseph Kabila, Profesa  Ernest  Wamba dia Wamba, Pierre Nkurunzinza wa Burundi, Yoweri Museveni, Waziri Mkuu wa Kenya, Raila Omollo Odinga, na rais Mstaafu Afrika Kusini, Nelson Rolihlahla ‘Madiba’ Mandela, Rais Mstaafu wa Msumbiji, Joachim Chissano, orodhas ni ndefu.
   Hayati Kabila, Garang na Samora ni miongoni mwa wanamapinduzi walioanzisha vuguvugu la ukombozi lililokuwa na kitovu  katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
Bahati mbaya sana , hawa mashujaa wamepokonywa uhai kwa vifo vya aina moja.Nuru yao imezima, wakati walipokuwa  wangali wakihitajika.
   Samora Machel, alikufa hivyo hivyo katika ajali ya ndege, Oktoba 19, mwaka 1986.
  Ilikuwa ndege aina ya Tupolev-134A. Ni Jumapili, saa tano hivi za usiku, ndgd hiyo ya Kirusi ikitokea Zambia , kupitia anga ya Zimbabwe , ili kurejea nyumbani, Maputo .
   Ndege hiyo ilianguka katika ardhi ya Afrika Kusini, ubavuni mwa milima ya Lebombo; ni eneo la Mbuzini; kwenye pembe ya Transvaal Mashariki. Ni jirani kabisa na mpaka wa Musumbiji, Swaziland na Afrika Kusini.
   Watu wengine 33 waliokuwemo katika ndege hiyo, pia walifariki dunia, wakati wengine 10 walinusurika.
  Kumbuka, Garang alipokufa walinusurika 13.Mwaka 1987 wakati wa Maadhimisho ya mwaka mmoja wa kifo hicho, Rais Joachim Chissano alisema, Komredi Machel hakufa kwa ajali; bali kifo chake kilitokana na hujuma.
   Duru za kipelelezi ziliutuhumu utawala wa Makaburu wa Afrika Kusini, hususan Shirika lake la Ujasusi la BOSS, kuhusika na njama za kifo hicho.Afrika Kusini iliunda Kamati yake ya Uchunguzi wa kifo hicho iliyokuwa chini ya Jaji Cecil Margo, wakasema marubani wa Tupolev 134A walikosea;wakadhani wanatua Maputo , kumbe walikuwa porini!
  Aghalabu, njama za mauaji ya wanamapinduzi hufunikwa kwa ‘magunia’ ili kuuficha ukweli.Hata mashujaa wanapouliwa kwa risasi ya kichwa, vyombo vya Habari  huambiwa “kalamu chini” halafu umma huambiwa ti ajali, Basi!
    Naam. Hata kifo cha Kanali Dk. John Garang kilifuatwa na tetesi kwamba kilipangwa.
  Rais "Seven Batallion" ama  Museveni, aliyedhamini safari ya Garang alikanushwa kifo hicho kutokana na hujuma zozote.
  Hivyo, Garang na Samora Machel, walikufa kifo kimoja.
   Wakati Garang alikwenda mjini Kampala kufanya mkutano na Museveni, Samora alikwenda mjini Lusaka kufanya mkutano na Rais Kenneth Kaunda wa Zambia .
  Kaunda alikuwa Mwenyekiti wa Nchi za Mstari wa Mbele wa Ukombozi Kusini mwa Afrika.
    Ni wakati huo huo kundi la kijeshi la RENAMO lilikuwa nchini Malawi. Enzi hizo Malawi iliongozwa na marehemu Dk. Hastings Kamuzu(kana-ka-Mzizi)Banda.
RENAMO walitumiwa kuidhoofisha Musumbiji baada ya uhuru, kwa sababu imesemwa Banda alikuwa kibaraka wa Wazungu.
   Mlinzi wa Samora, ambaye alinusurika katika ajali hiyo, Fernando Maniel Joao,alitambaa hadi katika kituo kimoja cha polisi, kuomba msaada ndani ya Afrika Kusini ya Makaburu.
  Joao anasema, wakajichelewesha kwenda kutoa msaada kwa majeruhi; hadi wakaja kutangaza baadaye keshoye kuwa Samora alikuwa amefariki.
  Polisi wa Makaburu walifika katika eneo la ajali saa chache baada ya habari, wakaishia kuiba nyaraka muhimu na kupora mizigo na fedha.
   Samora, aliongoza chama cha Frelimo(Mozambique Liberation Front), ambacho kilifanikiwa kupata uhuru, baada ya kuwang’oa Wareno mwaka 1975.
  Rais wa Uganda, Yoweri Museveni aliwahi kupata mafunzo ya medani ya kijeshi kwa wapiganaji wa Frelimo, kabla ya kurejea Uganda muda mfupi kabla ya Dikteta Iddi Amin Dada kumpindua Dk. Milton Apollo Obote, mwaka 1971.
    Baada ya mapinduzi, ndipo Museveni alipokuwa Dar es salaam na kusoma Chuo Kikuu cha Dar es salaam, shahada yake ya Sayansi ya Siasa(political science); akakutana na akina Garang, Kabila na wengine.
    Dk. Apollo Milton Obote, alianza kutawala Uganda kama rais Mei 24 mwaka 1966 hadi alipopinduliwa Januri 25 mwaka 1971 na Jenerali Amin, aliyekuwa Mkuu wa Majeshi ya Uganda. Obote, alirejea kutawala Uganda Desemba 1980 hadi Julai 27 mwaka 1985 alipopinduliwa kwa mara nyingine na Jenerali Tito Okello. Afrika, jua la Haki linakuchwa, zimebaki hujuma na njama za ‘makaburu mambosasa’ wanaohujumu kila haki na kila chanzo cha maendeleo ya watu.
 Leo, wanamapinduzi hawa wamepotea kuzimuni wakati harakati za mabeberu sasa wakitumia majeshi ya NATO(Northern Atlantic Treaty Organization) badala ya majeshi ya Makaburu na mashirika yao ya kijasusi kama BOSS,CIA n,k wanaipindua Afrika, ili kutwaa rasilimali zetu.
 Kisingizio ni demokrasia Afrika!
   Tunapomaliza  kuadhimisha miaka sita ya kifo cha Kanali Dk. John Garang de Mabior na uhuru wa Sudan,  tunashindwa kuthamini mchango wa baadhi ya viongozi wetu, wanaoonekana kama kondoo, lakini kumbe mbwa mwitu wakali.
  Leo,ukimwacha 'R.G' Mugabe, na Jacob Zuma Mushorozi, hakuna     tena wa kukemea ubeberu Afrika, akina Bernard Membe wanasema kwa kigugumizi juu ya uvamizi wa NATO, Afrika, naam Libya. Nani wa kuwakemea NATO dhidi ya vitendo vyao vya kupindua nchi na kuwasaidia Waasi?
   Dhana halisi ya ukombozi, haki, uhuru na maendeleo ya Waafrika husalia mbali.
Afrika itasemaje kwamba ilishinda vita vya ukombozi dhidi ya wakoloni, wakati wakoloni mamboleo wangalipo, ni vibaraka wanaoendeleza “NJAMA” mithili ya zile za Mashirika kama CIA la Marekani na BOSS, la Makaburu.
Leo, NATO wanatangaza amri ya 'No Fly Zone' hapa Barani pasipo AU kusema chochote. Mwanachama mmoja AU anapinduliwa na majeshi ya Wazungu kuanza kumsaka mithili ya panya,lakini hakuna wa kukohoa!
    Hawa, baadhi yao hufanya kinyume cha demokrasia na haki za binadamu;hufanya, “HUJUMA” na ufisadi.
Huonekana kana kwamba, ni “KIKOSI CHA KISASI” baada ya uhuru, na kuwapinga Wazungu kuendelea kujitwalia rasilimali za Bara letu na kupeleka chakula Ulaya, wakati watoto wa Afrika, wakipewa silaha wauane.
Leo, Libya kunaweza kufumuka vita ya wenyewe kwa wenyewe kwa muda mrefu,kwa sababu ndivyo NATO watakavyo,Afrika kusiwepo maendeleo na utangamano.
 Wamekuwa wakiwadhamini waasi wa Angola,Musumbiji, Sierra Leone na sasa Libya.
Baadaye huwatia mbaroni akina Charles Taylor na Fodday Sankoh ili kutuziba midomo.
   Tumeona Samora akihujumiwa na Makaburu.
  tuliona Patrice Emmely Lumumba akiuliwa na vibaraka, akina Mobutu na Moise Tshombe.
Tumemwona Kanali Garang akifa kwa ajali ya helkopta ya Museveni, mpakani mwa Uganda na Sudan.
Yumeona Afrika, baada ya uhuru wa vyama vingi, sasa majeshi ya kigeni yameanza kupukutisha serikali za Afrika kwamba ni madikteta, nasi tunashangilia sana bila kujua tunarejea zama za Makaburu na chini ya bendera za kikoloni kama Union Jack!
   Orodha ya waliokufa ni ndefu, ya waliokufa wakisaka mustakabali wa watu wao. Leo, mahakama ya mjini Hague imegeuka mahali pa kuwasweka rumande wengi WAAFRIKA tu, Wazungu wauaji kama Bush na Blair, hawakamatwi!
Hadi leo hakuna utangamano, kwa sababu WAZUNGU wangali wakimezea mate madini, samaki,  mafuta, madini,misitu,wanyama na rasilimali zingine.
Huwatumia viongozi wetu kuwa mawakala wa BOSS na CIA; wasomaji wakumkumbuke mwanamapinduzi Alstablus Elvis Musiba na vitabu vyake dhidi ya majahili hawa, ambao sasa wanaweka madarakani hapa Afrika viongozi, wanaotugeuka na kuuza kila kitu kwa bei bure.Hawa wanaokubaliana na uporaji-ubinafsishaji, ugenishaji na wizi wa rasilimali, hawakamatwi,wanaopinga kuhamishia rasilimali zetu Uswisi hukamatwa.
 Hata Nyerere aliambiwa kuiba fedha na kuficha Uswisi akagoma!Leo, wenye vijisenti wanaficha Jersey, halafu baadaye Wazungu husema kinafiki kwamba kuna fedha za Libya Ulaya,kwamba Mobutu alificha fedha Uswisi, huu ni wizi na utapeli tu.
    Wameuza migodi yetu na mashirika yetu kwa NJAMA za wakoloni, kwa kutumia Mashirika kama IMF,Benki ya Dunia na wahisani wengine, wanaojulikana kama G-8 n.k
   Ni kwa sababu hii Afrika inavuja damu mbichi, kuashiria adui yetu hayuko mbali nasi.
Afrika inateketea katika miali ya moto, kwa tamaa,rushwa,hujuma,ufisadi na kukosa haki.
   Madhumuni ya serikali za Afrika, yalikuwa kukuza Amani, Imani na Tumaini; isijekuonekana hili ni Bara la watu Bwana Mungu aliwaumba bahati mbaya.
Ndiyo sababu, viongozi ama watawala wetu wamekosa shabaha katika kila lengo la fursa za maendeleo duniani.
  Akina Nyerere, Kwame Nkurumah na wenzao walikuwa na visheni ya kutumia rasilimali na fursa za Bara hili, kuondokana na utumwa. Ingawa walishindwa bahati mbaya; waliondoka na njozi na malengo yao.
   Watawala walioirithi Afrika, wanaonekana kuikabidhi kwa wakoloni walewale; huku hawa wakijigeuza wanyapala.
Hawataki kuambiwa, hawataki uchaguzi, na hawana lengo la maendeleo kwa umma.
Ni waoga, wanapokea kila amri na shurti  kutoka Uingereza na Marekani kwa utii mkubwa.
Ni kwa sababu hii kuna ufisadi na kila machafuko.Shina la ufisadi ni Ulaya na Marekani.
   Hawa ni nani; kama si Kaini aliyemuua nduguye Abili kwa sababu ya choyo na tamaa ya madaraka?
Wapo viongozi wetu vitanga vya mikono yao vinachuruzika damu mbichi, kwa kuwaua Waafrika wenzao, Congo (DRC), Darfur, Sierra Leone  na mahali pengine pasipo amani hapa  Barani.
  Hata hapa kwetu kuna nyufa. Kelele za kuvunjika nyumba yetu zimesikika, mara “Oh..Bara wanainyonga         Zanzibar”, mara “Unguja anakula peke yake, wakati Pemba akiambulia makombo chini ya meza”, n.k
Wenzetu Kenya walikaribia kumalizana kwa tamaa ya ‘machungwa’ na ‘ndizi’.Somalia wanachinjana kwa sababu ya usultani na mamlaka.Vivyo hivyo ndugu zetu  Afrika Kusini wameanza kututimua nyumbani kwao, kwa sababu chakula kidogo-unga robo.
   I wapi leo thamani ya wimbo, “UHURU NA UMOJA”?
   Hapa, kuna siri ya maisha matamu-Furaha katika hali ya hewa ya kupendeza chini ya JUA LA HAKI lililokuchwa kwa sababu ya kiza cha dhuluma, tamaa ya madaraka,ufisadi, rushwa na choyo.Wenye nguvu huwapiga raia kwa ngumi za chuma. Akina Kaini!
   Palipo na giza hapana nuru; na palipo na nuru hapana giza.
BURIANI KANALI MUAMMAR AL GADDAFI, wamekuondoa,lakini angalau wewe ni Mwana wa Afrika!
      congesdaima@yahoo.com
        0786/0754-324 074
Top of Form
Bottom of Form
Top of Form
Bottom of Form
Top of Form
Bottom of Form