Friday, December 6, 2013

MANDELA BADO YU HAI HATA MILELE

MWANAHALISI wa Afrika, “The Great Son of Africa”, “Tata” Mandela, amepumzika kaburini baada ya kuwa mahututi tangu Juni mwaka huu.
 Ilikuwa vigumu Mandela kuishi katika hali ya maradhi mabaya ya mapafu na kupumulia mashine tangu awe mahututi miezi sita iliyopita.
Sasa,Mandela amefariki nyumbani kwake Desemba 5, saa 2: 57 usiku huko Johennesburg.
Binafsi,nilikuwa nimepoteza matumaini ya mtu huyu nimpendaye sana kuishi,japo afikishe miaka 100 kamili ifikapo Julai 18,mwaka 2018.
Nelson Rolihlahla ‘Madiba’ Mandela, alizaliwa Julai 18 mwaka 1918 katika kijiji cha Mvezo,katika Jimbo la Eastern Cape,Afrika ya Kusini.
Alikuwa mwanaharakati mashuhuri sana katika kupinga ubaguzi wa rangi wa Chama cha African National Congress(ANC)kinachoongoza sasa Afrika ya Kusini.
Miaka 27 ya uhai wake aliitumia akiwa jela,kufuatia harakati zake za kuwapinga Makaburu wa Afrika Kusini na siasa zao za Kibaguzi zilizoungwa mkono na Mataifa makubwa ya Magharibi.
Muda mwingi akiwa jela, akawa anaponda kokoto mchana wa hari akiwa hana viatu,hususan huko Kisiwa cha Robben,ambacho sasa ni kituo cha utalii.
Watu huenda kuona chumba alicholala shujaa huyu wa karne hapa Afrika na dunia nzima.
Namba yake ya jela, ‘46664’ itakaa kama ALAMA ya harakati za Ukombozi Kusini mwa Afrika, na katika harakati za uhuru hapa Barani.
Mtu huyu, ambaye sasa ni marehemu,aliachiwa huru na Makaburu Feburuali 11 mwaka 1990, na akawasamehe waliomsweka jela kwa jumla ya miaka 27.
Ni mzaliwa wa ukoo wa Thembu,katika kijiji cha Mvezo,wilaya ya Umtata,mji mkuu wa Transkei.Anatokana na ukoo wa Chifu Ngubenguka(alifariki 1832).
Babaye, Gadla Henry Mphakanyiswa(1880-1928) aliwahi kuwa chifu wa Mvezo,akapokonywa uchifu na wakoloni wa Kiingereza.
Mzee huyo alikuwa na wake wanne,akazaa watoto 13,Mandela alikuwa mtoto wa mke wa tatu,NESEKENI FANNY,Binfi wa Nkedama wa Mpemvu,wa kabila la XHOSA.
Jina la Rolihlahla maana yake ni ‘Kuvuta Tawi la Mti’ lenye kumaanisha ni mtu mwenye fujo!
Akiwa na umri wa miaka saba alikwenda shule, mwalimu wake aliposhindwa kutamka jina la Rolihlahla, akampa jina Nelson kwa heshima ya Mkoloni Mwingereza,Horatio Nelson.
Baba yake alifariki Mandela akiwa na miaka tisa tu; ikabidi sasa alelewe na rafiki wa baba yake.Mandela alisoma shule ya misheni ya Wesleyan.
Akaingia jandoni akiwa na umri wa miaka 16,kabla ya kwenda kusoma Clarke bury Insitute,alikotunukiwa cheti.
Aliwahi kucheza ndondi na riadha.Hapa namkumbuka mwanamasumbwi Nguli,Mweusi wa Marekani aliyetukanwa udongo wa mfinyanzi kufuatia kuwa Mweusi,Mohammed Ali.(Clay).
Mandela, alisoma Shahada ya kwanza katika Chuo Kikuu cha Port Hare, alipokutana na Mpigania uhuru mwenzake,Oliver Tambo.
Tambo, alikuja kuwa kiongozi wa ANC kabla ya kufariki dunia.Mandela aliwahi kuwa karani katika kampuni sheria mjini Johannesburg; alisaidiwa kupata kazi na Walter Sisulu.
Baadaye, alisoma sheria Witwatersand, ambako alikutana na wanaharakati wengine.Mandela na Oliver Tanbo waliendesha kampuni ya uwakili ili kuwasaidia Weusi waliokuwa wakikumbana na madhila ya kunyanyaswa na Makaburu.
Desemba 5, mwaka 1956 Mandela na wenzake walitiwa mbaroni na wenzake 150 na kushitakiwa kwa makosa ya uhaini-walishinda kesi hatimaye wakaachwa huru.
Johannesburg,ndiko aliswekwa rumande baadaye,baada ya kutafutwa sana na Shirika la Ujasusi la Marekani,Central Intelligence Agency(CIA).
Nataka msomaji,hasa vijana wa siku hizi kujua kwamba Marekani na washirika wake,waliwasaidia Makaburu na wakoloni wengine kuwahujumu Weusi wasije kujitawala siku moja katika nchi zao wenyewe.
Naam,leo hung’ata na kupuliza,na wajinga wote wanaona Mataifa haya ndiyo ‘Masihi’ na mabingwa wa demokrasia na Haki za Binadamu,kumbe ujinga mtupu!
Marekani na Shirika lake la CIA ambao hupigiwa goti siku hizi,wakishirikiana na Makabuu wa Afrika ya Kusini na tawala za Kiimla(Authoritarian) wakamshitaki Mandela kwamba alichochea mgomo wa wafanyakazi na kutoroka nchini kinyume cha sheria.
Yawezekana,ni wakati huu Mandela na wanaharakati wenzake walikuwa Mazimbu,Morogoro katika Makambi ya wapigania uhuru-Tanzania.
Oktoba 25 mwaka 1962 Mandela alihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela.Akiwa jela, huku nyuma polisi wa Makaburu waliwasweka rumande wanaharakati wengine wa ANC, akina Walter Sisulu,Govan Mbeki na wenzao.
Juni 12 mwaka 1964 wakahukumiwa kifungo cha maisha jela.
Kati kesi hiyo MANDELA pia aliunganishwa,wakapelekwa Kisiwa cha Robben mahali ambao Mandela akakaa miaka 18.
Kazi yao ilikuwa kugonga miamba na kuipasua ili kupata kokoto za kujengea jela imara sana za Makaburu ili wafungwa(WEUSI)wasitoroke.
Machi,1982 Mandela alihamishiwa Polls moor, akiwa na wenzake wa ANC akina Walter Sisulu.
Feburuari,1985 P.W.Botha, alimpa Mandela ‘Offer’ ya kuachiwa huru kwa masharti kwamba aachane na harakati za uhuru wa Mtu Mweusi.
Mandela alikataa ‘offer’ hiyo akatoa taarifa kupitia binti yake,Zindzi akisema:
“Uhuru gani ninaopewa wakati taasisi ya watu inabaki imepigwa marufuku? Hata hivyo,mfungwa hawezi kuingia mikataba!” Mandela aligoma kuachwa huru-uhuru bandia.
Wewe kijana wa sasa ulishaona wapi msimamo mkali wa Mwanahalisi wa Afrika (The Great Son of Afrika)  mithili ya MANDELA?
Makaburu WALIFANYA MKUTANO NA Mandela mfungwa mwaka 1985 Novemba, katika hospitali ya Volks, Cape town alipokuwa akitibiwa saratani-alikutana na waziri wa Makaburu,Kobic Coetsee.
Mwaka 1989,PW Botha aliugua kiharusi,nafasi yake ikachukuliwa na Frederic Willem de Klerk,rais wa Kwanza Kaburu Barani Afrika, wenzake walikuwa Mawaziri wakuu, akatangaza kuwa Mandela angekuwa huru mwaka 1990.
Waafrika tukafurahi,mtu huyu kipenzi cha watu kuwa huru
.Alipewa nishani ya Amani ya Nobel,yeye na De Clerk mwaka 1993.
Baadaye Makaburu walimuua Chris Hani,Aprili 1993.Mandela alikuwa rais Afrika ya Kusini akiwa na miaka 77 mwaka 1994, akaja kustaafu mwaka 1999.
Aliapishwa kuwa Rais wa kwanza Mweusi wa Afrka ya Kusini Mei 10, mwaka 1994,de Clerk akawa Makamu wa Kwanza wa rais na Thabo Mbeki akawa Makamu wa Pili katika serikali ya Umoja wa kitaifa kama ya Zanzibar hivi.
Utawala wa Makaburu(Boers)ulikumbatiwa na Uingereza na Marekani;wakati watu zaidi ya 14,000 (Weusi)walipouliwa huko Zulu,katika miaka ya 1980.
Tumeona Mobutu akisaidiwa na mataifa haya ambayo siku hizi hujidai ‘Masihi’ hapa duniani,na huimba demokrasia na Haki za Binadamu kwa midomo bila vitendo.
Mobutu,na hawa,waliwasaidia Waasi wa Angola kukipinga Chama cha Ukombozi, Popular Movement for the Liberation of Angola(MPLA),uhuru usipatikane kutoka kwa Wareno,hadi nchi ikabaki vitani kwa muda mrefu.
Mobutu na hawa rafiki zake, Ungereza na Marekani, walimsaidia Jonas Malheiro Savimbi na Chama chake cha Unita, kilichopinga uhuru wa Angola.
Tumeona harakati za uhuru nchini Afrika ya Kusini chini ya African National Congress (ANC) zikiwa zimeharamishwa na utawala dhalimu sana wa Makaburu hadi Rais De Clerk alipokuja kuondoa marufuku hiyo Feburuari 1990
“Tata”Mandela aliachiwa huru kutoka Greza la Victor Verster, lililopo Paarl Feburuari 11 mwaka 1990. Ni tukio la kihistoria kuachiwa kwa Mandela; ni kama Afrika ilipata uhuru mwaka 199
Mtu huyu, “Tata” Mandela,alitangaza msamaha kwa Makaburu waliomtesa; ikaunfdwa Tume ya Ukweli na Maridhiano(THE TRUTH COMMISSION) iliyoongozwa na Askofu Desmond Tutu.
Mandela alikiri chama chake (ANC) kuunda tawi la jeshi(Umkontho we Sizwe) kwa nia ya kujilinda na kujihami dhidi ya siasa za ubaguzi wa rangi; siasa zilizoandamana na dhuluma na mauaji ya kinyama dhidi ya wazalendo na harakati za ukombozi.
Mandela na De Clerk walitunukiwa baadaye tuzo ya Nobel ya Amani,mwaka 1993.Aprili mwaka huo 1993 ndipo Mpigania uhuru Chris Hanni alipouliwa na utawala wa Makaburu,rafiki wa Uingereza na Marekani.
Mandela, ameishi siku zote kama Mwafrika halisi; akachaguliwa kuwa rais mwaka 1994   akiwa na umri wa miaka 77-na alistaafu mwaka 1999 akamwachia kiti Thabo Mvuyelwa Mbeki,mmoja wa wana wa mashujaa wa mapambano dhidi ya Kaburu jeuri.
ANC kilishinda uchaguzi wa 1994 kwa asilimia 62 ya kura.Mandela aliapishwa kuwa rais wa Kwanza Mweusi Mei 10,mwaka 1994,wakati Kiongozi wa National Party, de Clerk akiambulia Umakamu wa Kwanza wa rais;wakati Thabo Mbeki alipopewa Umakamu wa Pili katika serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Naam, tunamkumbuka ‘Tata’Mandela kwa mashati yake ya Batiki.
 Ama ‘Mandela Shirts’ yanayovaliwa siku hizi hata na akina Rais Jakaya Kikwete.
Uchaguzi wa kwanza huru Afrika ya Kusini ulifanyika Aprili 26-29,mwaka 1994,ANC kikapata asilimia 62,National Party cha Makaburu kikapata asilimia 20.4.Inkhata Freedom Party cha Chifu Mangusuthu Butelezi kilipata asilimia 10.5.
‘Tata’ Mandela alipata kuoa mara tatu; ni baba wa watoto sita,wajukuu 22 na vitukuu vingi. Mmoja wa wajukuu zake ni Chifu Mandla Mandela.
Mzee huyu kipenzi cha Afrika alifunga ndoa ya kwanza na Evelyn Ntoko Mase kutoka kwao Mandela huko Transkei.Walikutana Johannesburg-walizaa wavulana wawili,Thembikile ama Thembi mwaka 1946,Magkatho alizaliwa 1950 na wasichana wawwili waliopewa jina moja,Makaziwe, “Maki” mmoja alizaliwa 1947 na mwingine 1953.Mwingine alifariki dunia kabla ya kufikisha umri wa mwaka mmoja.
Ndoa ya Mandela na Evelyn Mase ilivunjika baada ya miaka 13(mwaka 1957),Mandela alikuwa haonekani nyumbani kwa muda mrefu,akiwa ‘Msituni’katika harakati za Ukombozi,mama huyo na imani yake ya kilokole ya Mashahidi wa Jehova, aliamua kwenda zake,akaachana na Mandela.
Thembi, alifariki katika ajali  ya gari mwaka 1969 akiwa na miaka 25 wakati huo Mandela alikuwa selo, Robben Kisiwani.Hawa watoto walisoma shule moja,baadaye Evelyn alifariki dunia 2004.
Ndoa ya pili ya Mandela ni ya Winnie Madikizela-Mandela, huyu ‘Iron Lady’ kutoka Transkei.Watoto wa Mandela na Winnie ni wasichana wawili:
Zenani au Zeni(Feburuari 4,1958) na Zindzishwa ama Zindzi aliyezaliwa 1960.
Walitengana Aprili 1992; mwaka 1996 waliachana kabisa.Juzi, Winnie alikwenda kumtembelea  Mandela hospitalini anakolazwa.
Kaka mkubwa wa Mfalme wa Swaziland,Mswati III,Prince Thumbumuzi Dlamini alimuoan Zenani mwaka 1973,na wanaisti Boston,Marekani.
Mwaka 1998,Mandela alimuoa Graca Machel nee Simbine wakati alipokuwa akiadhimisha ‘Birth Day’ ya 80.
Mwaka 2003,Cable News Network(CNN) walitangaza tanzia ya Mandela.Mwaka 2007 pia ‘wasela’walitangaza kifo cha Mandela,wakiwataka Wazungu kwenda kwao,la sivyo wangechinjwa!
Mtu huyu, ‘Tata’ Nelson Mandela ni kielelezo cha Mzalendo wa kweli,Mwanahalisi wa Afrika aliyeitwa ‘Gaidi’ na utawala wa Makaburu wa Waziri Mkuu PW Botha, aliyejiuzulu Agosti 14, mwaka 1989 ndipo akaingia De Clerk aliyemwachia huru Mandela.
 Utawala wa Makaburu uliua watu wengi,si Afrika Kusini tu bali hata Msumbiji walifanya njama na kumuua Samora Machel mwaka 1986.
Naam,namkumbuka ‘Tata’Mandela, ambaye namba yake ya jela ilikuwa 46664. Tunawakumbuka wanamapinduzi wa Afrika ambao wamemwaga damu wakipigania uhuru wa watu wao, si ulaji wa matumbo  yao kama watu wengine wanavyotaka kuitwa leo.
Namkumbuka Samora Moises Machel,John Garang de Mabior ‘ Chris Hani na wenzao.


No comments:

Post a Comment