Wednesday, November 13, 2013

habari zenu nazo!



RAIS THOMAS JEFFERSON, wa Marekani(1801-1809) aliposhambuliwa sana na magazeti, wakati wa Awamu yake ya Tatu ya utawala wa Taifa hilo kubwa duniani, alisema hivi:
   “Mtu asiyechungulia kabisa katika kurasa za magazeti ,yu na taarifa sahihi kuliko anayesoma magazeti hayo kila siku. Maana yake ni kwamba, asiyejua chochote yu jirani na ukweli, ukilinganisha na yule ambaye akili zake zimejazwa uongo na upotovu”.
   Hii ni barua ya Rais Jefferson, kwa John Norvell, Juni 14, mwaka 1807.
 Hapa,  nakusudia kusema kwamba, mtu mzito sana katika nchi inayoongoza kwa demokrasia duniani, na uhuru wa vyombo vya habari, akavilaumu na kuvilaani sana vyombo hivyo, kwamba heri visingekuwepo aslani.
    Mwahahistoria wa Kiingereza, Thomas Babington Macaulay, ndiye aliyevibatiza vyombo vya habari wadhifa mtukufu wa “MHIMILI WA NNE WA DOLA”.
 Vyombo vinavyolalamikiwa kuwaongezea  mahluki ujinga, hadi watu wakubwa namna hii wakasema, ‘Heri visingekuwepo’!
Ni vyombo hivi vinavyowapigia debe wakubwa kuingia kwenye ulaji, halafu vinapoanza kuwaponda.vinageuka ‘Shetani’ kheri visingekuwepo duniani?
  Spika wa zamani wa  Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta, na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo wa zamani, George Mkuchika, zamani kidogo walilaumu baadhi ya magazeti(siyo Mwanahabari), kana kwamba ingekuwa heri wananchi kutojua kitu chochote, kuliko kuyasoma magazeti hayo,ili kujazwa ujinga!
   Sitta na Mkuchika wanakubaliana na Thomas Jefferson kwamba,
   “The man who never looks into newspapers is better informed than who reads them inasmuch as who knows nothing is nearer the truth than he whose mind is filled with falsehood and errors”.
   Yapo mambo yaliyoandikwa na magazeti ,yametia ukakasi katika vichwa vya mihimili mingine ya Dola, yaani Bunge na serikali.
 Bila shaka magazeti hayo yalibeba ajenda za wahariri na wamiliki wake, waandishi na zaidi sana yalitafuta kupambana na matatizo binafsi ya kisiasa(political problems) zaidi ya kufahamisha na kuelimisha umma.
Lakini, wakubwa huwa hawataki kuelezwa udhaifu wao,wanataka sifa tu.
    Waziri mwenye dhamana ya Habari, wakati huo George Mkuchika,  alitishia kutumia ‘rungu’ alilopewa na Katiba kutaka kufungia magazeti hayo.
Hata siku hizi za akina Fenela Mkangala,magazeti yalishafungiwa,yanagugumia kwa maumivu,ingawa mwanzoni mwa Kikwete yalisemwa kumlamba miguu rais!!
Kufungia vyombo vya habari?
  Kwa sababu, kufanya hivyo si kuchimbua mizizi ya tatizo la ukiukwaji wa maadili ya taaluma ya Uandishi wa Habari nchini. Ni kufukia uoza usionekane, tena kuahirisha riha mbaya ya uandishi isifike puani mwa wasomaji.
   Lipo tatizo la msingi la baadhi ya watu wanaotuhumiwa kuhusika na ufisadi, kwamba wamesajili magazeti yao ili yafunike madhambi yanayosemwa sana juu yao .
   Ushahidi unaoonekana ni kwamba baadhi ya magazeti siku hizi yamekuwa yakimshambulia mtu mmoja kiasi kwamba ni nadra kukuta ‘Maslahi ya Taifa’ ndani ya mashambulizi hayo.
   Nachelea kumuunga mkono Mfanya biashara, Reginald Mengi, na kauli zake kwamba, ‘Mafisadi wameanzisha vipeperushi’ ili kumshambulia, kwa sababu hata yeye mageti yake ya Taifa Letu na Sema Usikike, yametajwa na Waziri Mkuchika kuandika habari zinazotia kichefuchefu!
    Sina hakika kama wakati ule ofisi ya Waziri Mkuchika ingeweza kuingia mkenge, ikasajili vipeperushi zaidi ya magazeti, wakati kuna sheria, kanuni na taratibu za kusajili magazeti.
 Sheria hizo huainisha magazeti, vipeperushi, majarida n.k
    Niunge mkono hoja kwamba yapo magazeti yaliyoanzishwa karibuni, yana lengo la kunyamazisha kelele za umma dhidi ya ufisadi na mafisadi kwa njia ya kutangaza ‘Privacy’ za watu, ili wasahahu kwamba kuna mafisadi.
Mengine huanzishwa na wanasiasa kuelekea 2015.kazi ni kuudanganya umma na kuwachafua adui zao wa mapambano ya siasa.
   Magazeti ya kale yamekuwa yakiandika kwamba kuna watu wanatumia vibaya madaraka waliyopewa, wanakiuka maadili ya uongozi na kutumia vibaya rasilimali za umma.
   Wakati, magazeti ya sasa yanajaribu kutwambia kwamba wapigao kelele sana dhidi ya ufisadi ni ‘mabingwa wa kuoa na kutaliki’; tena wapo vigogo ni ‘manchampioni’ wa kuwaweka kinyumba wanaume wenzao, naam mashoga!
   Bila shaka hivi ni vita kati ya mtu na mtu, kati ya kundi moja na jingine.Yapo magazeti hayana ajenda,ila kutangaza pumba,yanaapisha!
 Hata hivyo, wapigao ‘panda sana ’ hawana tofauti kubwa sana na kigenge cha matapeli, ambao licha ya kuendesha kampeni dhidi ya wapigao kelele dhidi ya ufisadi, huwadhulumu sana waandishi; huwapiga ‘danadana’ kila kunapokucha.
    Vyombo vya habari vina jukumu begani mwake kufichua uovu na uhalifu. Vyombo hivi ni Kioo cha Jamii.
Kazi ya kioo ni kuonesha uso ama sura ya mtazama kioo.Kukosoa kwa nia ya kujenga Taifa imara na safi.
   Kioo hakimsingizii mtu makasoro yake. Kioo hakimsemi mtu kwamba ana kunyanzi ama udelele na madevu mithili ya shamba la Miwa la Kilombelo, wakati hana.Kioo hakiwezi kusema kwamba Shetani ni Mungu na Mungu ni Shetani ama Obama ni Osama, ingawa majina yao hufanana na hulingana kasoro herufi ‘B’ na ‘S’ katikati ya majina yao.
Vyombo vya habari hutakiwa kuwa makini na wakweli na walinganifu.
   Kazi ya kioo ni kusema ukweli kama fisadi anayo matongotongo, udelele, makunyanzi na hata midevu inayotisha watoto na kuonja michuzi.
   Mtazama kioo, awe na udelele, tongotongo, makengeza ama makunyanzi, hapaswi kukasirika na kukivunja kioo chake pindi kimwonyeshapo taswira ama mwonekano wake. Anapaswa kutumia maji na sababuni kujitakasa.
    Mafisadi hawataki kujitakasa  ili waonekane safi mbele ya kioo na mbele ya jamii.
Wanavunja kioo halisi, kisha hutengeneza vioo feki na bandia ili kuwageza wananchi kuona makengeza na maruweruwe!
   Nataka kusema kwamba, wakati maadili ya uandishi wa Habari yanataka habari ziwe ‘Objective, Fair na Accurate', siku hizi twasoma habari za kushambuliana, kutetana na kulumbana  wenyewe kwa wenyewe.Tunasoma ushabiki mwingi. Upuuzi,vita uongo na chuki na uchimvi hasa kwenye mitandao ya kijamii.
   Zaidi sana , twasoma ‘kati kati ya mistari’ wamiliki wa magazeti hayo wakimwagiana uvumba, matusi na fitina ili kuvuana nguo na kubakizana utupu-uchuro na mambo ya kijingajinga!
   Tunauliza:
 “How can they balance freedom of the press with the rights of individuals to privacy and their good names?”
   Lini uhuru wa Habari ulifikisha mwisho Haki za watu zinakoanzia, hadi tuambiwe mambo ya kupigana denda wakati hayahusiani kabisa na ajenda ya wizi wa mali ya umma?
    Waama, huu uandishi wa ‘sensationalism’ na vita dhidi ya mtu na mtu au kundi moja linalojidai safi dhidi ya jingine linaloitwa fisadi, faida yake nini kwa umma wa Watanzania?
   Heri magazeti haya yasingekuwepo, kama alivyosema Rais wa Tatu wa Marekani, Thomas Jefferson..
   Mhimili wa nne wa Dola(vyombo vya habari) una dhima ya kuonyesha makosa ya watu na serikali yao katika kujiletea mafanikio. Vyombo hivi vifanyapo kazi sawa sawa ni  kama kioo cha kuonyesha watu wapi wana mapungufu, ili wayarekebishe.
  Naam, vyombo vya habari ni sawa na kioo kikubwa ukutani, ambacho watu wote wan chi hupita kujitazama.
    Ni aibu kundi Fulani la watu( sijui ndiyo mafisadi kweli) wanapojitazama katika kioo hiki kilichopo njia kuu, hubaini tabia zao chafu, lakini badala ya kujisafisha udelele na tongotongo, huwaleta  mafundi vishoka ili wakavunje kioo kinachoonyesha makunyanzi na  makengeza yao na kutengeneza vioo vipya vipya feki.
   Lengo ni kuwachanganya watu wasione makunyanzi na matongotongo yao ? Lengo ni kuifanya jamii ya Tanzania iwe makengeza?
   Nakusudia kusema kwamba, hawa hawana nia nyingine ila kutaka umma wa Watanzania useme kwamba vyombo vya habari vya Tanzania (kioo cha jamii) havina maana kwa kuwa vimejitia unajisi na vinachafua watu badala ya kuonyesha kasoro.
   Watu hawa, wanataka umma wa Watanzania uone kwamba ni heri kutosoma magazeti kabisa kuliko kuyasoma na kujazwa ujinga!
 Kwamba, eti mawaziri wetu wakuu wanapostaafu, hujitwalia madume menzao kuwa ‘vimada’ wao; kwamba Tanzania kuna ma “Retired” PM(But not tired) viwembe 'Chapa mamba' katika ngono za jinsia moja! Uchuro.
    Nazungumzia ulazima wa kuwepo ama kutokuwepo kwa vyombo vya habari, kama habari zenyewe zinatia ukakasi kiasi cha macho kupatwa kiwi na meno kuota ganzi!
  Thomas Jefferson, kabla ya kuwa Rais wa Marekani alimwandikia barua Kanali Edward Carrington, Januari 16, mwaka 1787 kusema, angepewa kuamua kuhusu kuwepo au kutokuwepo vyombo vya habari asingesita kuchaguwa kuwepo kwa vyombo vya habari hata mahali ambapo hakuna serikali.
   Vyombo vya habari vifanyavyo kazi sahihi ni muhimu kuliko serikali.
Ewe Fisadi, unapovunja ‘Kioo’ nani akuoneshe udelele wako? Tatizo siyo kioo, ni udelele na ufisadi(uchafu) wako. Je, kioo bora kisiwepo ili udelele wako usionekane?
   Vyombo vya habari(kioo) ni muhimu kuonyesha uchafu wa mafisadi, ili wajisahihishe.Waache kujenga chuki dhidi ya kioo kionyeshacho makunyanzi na udelele wao.
      0786/0713-324 074

No comments:

Post a Comment