Monday, October 22, 2012

MAUAJI YA KAMANDA BARLOW-FULL STORY 2



                       
JULAI 28,mwaka 2003, aliyekuwa Mkuu wa kituo  kikuu cha Polisi  (OCS) Jijini  Mwanza, Daniel Maburuki Mahende(45) aliuawa  kwa risasi na majambazi,katika eneo la Bugando,jijini Mwanza.
Serikali iliahidi kuwatia mbaroni wauaji hao, waliohisiwa majambazi kutoka Burundi. Haikujulikana baadaye kwamba wauaji hao walichukuliwa hatua gani na mahakama.
Mwanza,kumetokea matukio ya mauaji ya kinyama sana.Lakini umma haukujulishwa hatua zilizochukuliwa dhidi ya wahusika ili liwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama zao.
Katika makala yaliyotangulia, nikaeleza kwamba, aliwahi kupigwa risasi ya kichwa ‘cashier’ wa Tanzania Breweries Limited(TBL),Pasiansi, Jijini,zikaporwa zaidi ya shilingi milioni 200.
Baadaye,nilipomuuliza aliyekuwa Wakili wa Serikali Mfawidhi,katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP)Kanda ya Ziwa, Anselm Mwampoma, akaniambia:
“Kesi hiyo ya mauaji ya ofisa wa TBL,huko Pasiansi,haikuwa na ushahidi wa kutosha kuwatia watuhumiwa hatiani”, alisema Mwampoma.
Tuseme, kesi hiyo “Ilivurugwa” ama ilichakachuliwa,hata ushahidi uliokuwepo haukutosha hata kuwafikisha mahakamani washitakiwa. Hili Mosi.
Pili, aliyewahi kuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Mwanza,(RCO) Goodluck Mongi, aliwahi kusema katika semina iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU) kwamba wapo maofisa wa Mahakama Mwanza, waliwahi kumtorosha mtuhumiwa wa ujambazi ,gerezani Butimba,kwa ‘removal  order’ akatoweka rumande, na siku ya kesi mahakamani mshitakiwa  hakuonekana!
 Yaani, wakati maofisa wa polisi wakihaha kumfikisha mtuhumiwa wa ujambazi mahakamani, alishayeyuka rumande!
Sipendi kusema kilichotokea, lakini msomaji unaweza kujua inakuwaje mtuhumiwa wa ujambazi anapewa dhamana, kwa “removal order” ya   Mheshimiwa Hakimu, pasipo hata polisi kujua?
Kuna matukio lukuki  ya ujambazi Mwanza,wizi,uhalifu,mauaji ya kutatanisha n.k Hata hivyo, umma haujui kwa nini wahusika hawajakamatwa na kufikishwa mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake.
Hii ni HATARI!! Matukio ya karibuni sana ambayo hata Marehemu Kamanda Liberatus Barlow aliyashuhudia,ni ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Gazeti la Kasi Mpya, Richard Masatu, ambayo licha ya ripori ya daktari kuoneshwa kuwa aliuawa, polisi waliendelea kusema aligongwa gari!
Kuna mauaji ya mmiliki wa nyumba moja ya wageni Jijini Mwanza anayejulikana kwa jina la Manumbu, aliuliwa kwa risasi,lakini umma haujafahamu kilichotokea, na wala hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Kuna kawaida ya matukio ya mauaji kutokea Mwanza,lakini sijui polisi wanashindwa kuwabaini wauaji ili wafikishwe mahakamani?
Kuna watu wanakufa katika mazingira ya kutatanisha,lakini mwisho wa siku hakuna mtu anayekamatwa na polisi ili ashitakiwe mahakamani.
 Mwanza,kuna historia ya Mbunge mmoja, kumwagiwa tindikali,lakini ‘kesi iliyeyuka’ kwa njia zisizofahamika,kufuatia mtuhumiwa kuyeyuka,kama walivyoyeyuka  mashahidi wa kesi ya mauaji ya aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa huko Kenya,zama za NYAYO,Dk.Robert Ouko.
Aliyekuwa Meya wa Jiji la Mwanza, Leonard Bihondo, alituhumiwa kumuua aliyekuwa Katibu wa CCM wa Kata ya Isamilo, Bahati, alitiwa mbaroni na kesi yake ingali ikisubiri kuanza kusikilizwa.
Jumatano, Oktoba 17,mwaka huu,nikaazimu kumuuliza Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini(DCI)Robert Manumba,kama alijua mauaji ya Kamanda Barlow yalifuatiwa na mauaji ya watu wengine hapo Mwanza,lakini haikufahamika hatma ya mauaji hayo?
Na kwamba, Je, polisi wamefikia hatua ya ku  “compromise” na hali hiyo? Nilimkuta Robert Manumba,mbele ya jengo la ofisi ya Kamanda wa Polisi Mwanza,nikamsalimia kasha nilipomgusia jambo hilo akaniambia:
“Rafiki yangu,mimi ni mgeni hapa! Wenyeji mbona wapo ofisini unaweza kuwauliza hata wakasema kuhusu kilichopo?’ Manumba aliniambia. Nilicheka,kasha nikamuaga,maadam alikwisha pangua ‘ngumi’ za uso nilizotaka kumtupia!
Nilimpata Mkuu wa Upelelezi (RCO)Mkoani Mwanza,Mrakibu Mwandamizi wa Polisi(SSP)Joseph Konyo(siyo Joseph Kony wa  Lord’s Resistance Army wa Uganda).Siku hiyo, Oktoba 17,nikamwambia Joseph Konyo, juu ya migogoro Rwanda,Burundi na Jamhuri ya Congo(DRC) ilivyosababisha wakati Fulani huko mkoani Kigoma bunduk,SMG,i kuuzwa kwa kubadilishana na  DEBE LA MAHINDI au MTAMA!
Nilimuuliza Konyo, kama hakujua kwamba wakati Fulani wananchi kutoka Kigoma walihudhuria semina moja ya Upunguzaji silaha, wakasema  Mwanza ndilo lilikuwa soko kuu la silaha?
Na kwamba, polisi waliposhindwa kuchukua hatua sasa silaha haramu zinapatikana mikononi mwa wahalifu hata kuweza kuua raia na hata maofisa wa polisi kama Kamanda Liberatus Barlow?
“Nilikuwa Kigoma, wakati huo mwaka 2004,iliposemwa kwamba bunduki moja ya SMG ilibadilishwa kwa debe la mtama au mahindi katika magulio.Haikuwa na ushahidi kwamba wanunuzi wa silaha hizo walitokea Mwanza, hata hivyo polisi lazima washirikiane na raia ili kutokomeza uhalifu”, Joseph Konyo alisema.
“Nawashauri raia wema wa Mwanza,wasiache kushirikiana na polisi ili kusaidia kuondoa kitisho cha amani. Bila amani,hakuna kitakachofanyika. Wasikate tamaa,raia wanapaswa kutoa taarifa hata katika ngazi za juu za polisi,wanapaswa kutuamini kama wanataka tupambane na uhalifu na kuushinda”, Konyo alisema.
Akasisitiza kuwa, kumkamata mtuhumiwa ni jambo moja,lakini kumfikisha mahakamani na kuthibitisha kosa, ni jambo la pili linalohitaji ushiriki wa raia wema kutoa ushahid, ili kuthibitisha kosa pasipo shaka yoyote.
Nikamkumbusha RCO,Konyo madai ya wananchi wa Mwanza,kwamba wakitoa taarifa za uhalifu,mara wahalifu hukamatwa kasha kuachwa huru ambapo kitendo cha raia kuwajulisha polisi wahalifu hugeuka jambo hatari kwa maisha yao?
Siku tano baadaye, RCO,Joseph Konyo akafanya mkutano na maofisa wa Polisi na kuwataka kushirikiana ipasavyo na wananchi katika vita dhidi ya uhalifu nchini.
“Polisi tunapofuatilia uhalifu,tunapowajibika ipasavyo katika matukio ya uhalifu,tukishirikiana na raia wema tutatokomeza uhalifu”, Konyo alisikika akiwaambia maofisa wa Polisi.
Mkutano huo,ulihusisha maofisa wakaguzi wa polisi, maofisa wa idara ya upelelezi na maofisa wa kawaida.
 Kauli hiyo ya Konyo imekuja siku chache baada ya kifo ca Barlow, ambaye pia ameuliwa katika mazingira ya kutatanisha, ambayo raia wanadhani kulikuwa na uzembe na tabia ya kuwalea wahalifu iliyojengwa muda mrefu hata kusababisha mazingira ya ‘Mdharau Mwiba Guu likaota tende!”
Kufuatia hali hiyo, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Nchini,Robert Manumba, anasaidiana na makachero wa Polisi wa Kimataifa, Interpol, kuwawinda majahili hao waliomuua Barlow,na inshallah, baada ya kitambo watakuwa wametiwa mbaroni na kufikishwa mbele ya sheria.
Hadi sasa watu takriban 15 wamehojiwa na polisi,na watu kadhaa wanashikiliwa kufuatia mauaji hayo ya kuamkoa Jumamosi,Oktoba 13, majira ya saa 7-8 huko Kitangiri.
Mwanza ni mahali ambapo motto aliwahi kutekwa nyara, watekanyara wakaomba wapewe mamilioni ya fedha ili wamwachie mtoto huyo. Uliwahi kusikia hadithi za utekaji nyara na watekaji kuomba fedha nyingi za ‘kikombozi’?
     Haili liliwahi kutokea huko Bwiru,mtoto akatekwa nyara, wateka nyara wakaomba pesa, polisi walipojaribu kumwokoa wakishirikiana na babaye, mtoto alitoswa Ziwa Victoria na kufa!
Haya mambo ya Palestina, Ulaya na Afghanistan,yaliwahi kutokea bwiru,Mwanza. Mwanza watu waliwahi kuteka msichana wa baa,wakachinja, wakachukua kichwa,shavu la kulia wakanyofoa sehemu zake za siri,kasha kiwiliwili kikasokomezwa kwenye sandarusi na kuachwa penye pagala!
Wauaji wengine walitoroka,polisi hawakuwahi kuwakamata na kuwasweka hata rumande. Hapa Mwanza, ndipo mahali ambapo mwanamke anachinjwa chumbani, hata majirani wakashindwa kujua hadi walipoalikwa na mainzi ya kijani asubuhi,maiti akiwa ndani ya kiroba,katika pagala la mitaa ya Kiyungi!
Hapa ndipo jamaa mmoja wa Kenya alitaka kumuuza albino kwa shilingi milioni 400,ikawa bahati polisi wakamnasa na kumwokoa albino aliyekuwa hatarini kuchinjwa ili viungo vyake vikauzwe kwa watu wanaotaka utajiri kwa kutumia  ‘ndaku’ au bahati Fulani za utajiri.
 Huku ndiko albino huwindwa kama wanyama,hata sasa wapo wanaoishi katika kambi maalum wasije kuuliwa. Hapa ndipo vikongwe wanauliwa kwa tuhuma za ushirikina.
Hapa ni mahali ambapo wahalifu wana ‘confidence’ hata walipomaliza kumuaa Kamanda Barlow, walitoroka na Radio Call na bastola yake.Walivalia majazi ya polis Jamii.Waliyatoa wapi?
Hata hivyo, katika medani ya upelelezi,ni mapema mno kusema nani alimuua Kamanda Barlow ambaye tayari amezikwa kwao Kilimanjaro.
Katika medani ya ukachero,siyo kila anayekutwa na kamba shingoni akiwa amekufa,basi kajinyonga! Polisi wana kazi ya kuchuja habari,kuzikagua na kugundua wahalifu wapya,kasha kutafuta ushahidi na kuutetea mahakamani,ili  kuithibitishia mahakama pasipo shaka yoyote(beyond reasonable doubt) kwamba muuaji ni Fulani.
Itaendelea


No comments:

Post a Comment