Thursday, April 11, 2013

Mbumbumbu kutunga Katiba ya Tanzania!!



                                      
AWAMU ya Pili ya kuratibu na kukusanya maoni ya wananchi itafanywa kupitia Mabaraza ya Katiba.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba itaratibu na kukusanya maoni ya wananchi kupitia Mabaraza ya Katiba katika ngazi anuwai,kabla ya maoni hayo kuwasilishwa Makao Makuu,kwa ajili ya tathmini na kuandaliwa Ripoti.
Mabaraza ya Katiba yanatakiwa kutoa maoni juu ya Rasimu ya Katiba na kujadili ili kutoa maoni kwa kupitia mikutano itakayoitishwa na Tume ya Katiba,ili kushirikisha na kukutanisha wawakilishi toka makundi mbalimbali ya wananchi katika jamii.
Kufuatia hali hiyo,uchaguzi wa wawakilishi ama wajumbe wa Mabaraza ya Katiba unafanywa. Niseme wazi kuwa uchaguzi huo unatia kinyaa.
Napenda kumhadharisha Mwenyekiti wa Tume hiyo,Jaji Msitaafu,Joseph Sinde Warioba na wenzake kwamba, wajumbe wa Mabaraza ya Katiba hususan wale wa kata, wengi wao ni kichekesho cha mwaka!
Wamechaguliwa kwa kuhonga vijisenti,na wengine walichaguliwa kwa upendeleo wa udini na ukoo,kiasi kwamba inatia shaka kama hata Katiba wanaijua na umuhimu wake!
Vijijini,rushwa za kijinga zimetumika ili kuwapata wajumbe wa Mabaraza hayo ya Kata; kwani mfumo mzima umeendeshwa kimbumbumbu,pasipo hata wasimamizi kujua ni aina gani ya watu walihitajika kuchaguliwa ili wawawakilishe wenzao katika kupitia Rasimu ya Katiba na kutoa maoni yao.
Jaji Warioba, aamini ama asiamini,wajumbe wengi wa Mabaraza hayo ya Kata.hawaelekei kufahamu chochote juu ya Katiba na umuhimu wake.
Bali, wamechaguliwa kutokana na ujanja ujanja ili wajipatie posho,ambayo inasemekana ni kubwa,ili kujiongezea kipato.Kilichowasukuma kuanza kuhonga wajumbe, si weledi ama ujuzi na nia ya kutoa maoni,bali kusudi ni kujipatia posho inayotolewa na Tume.
Kama ingewezekana, wajumbe wote wangepewa mtihani ili kupima uelewa wao japo kidogo tu kuhusiana na Katiba na Misingi yake kama Haki za Binadamu na Utawala Bora.
Hatuwahitaji watu waliouza mbuzi na kuku na kuhonga honga wananchi na wajumbe wa Mabaraza ya Kata(WDC) mwisho wa siku,Tume ya Jaji Warioba itakumbana na kituko cha mikutano ya watu wa ajabu wasio na ufahamu juu ya mahitaji ya msingi ya wananchi wenzao,isipokuwa wamelipwa posho za mikutano na kujiondokea.
Kulingana na Tangazo la Serikali Na 394 la mwaka 2011 Sheria Na 2 ya mwaka 2012 kifu.3, Mabaraza haya yanayoundwa na raia wa Tanzania yangepaswa kuwa na mawazo ya Watanzania,badala ya kuwakilisha kiu ya posho,njaa na uzalendo wa matumbo yao badala ya uzalendo kwa taifa letu.
Kuhonga wananchi vitu vidogo vidogo ili wachjaguliwe kushiriki Mabaraza hayo pasipo wengine kujua na kusoma, ili wakapitia Rasimu ya Katiba,ni kichekesho cha mwaka.
Nimezungumza na wananchi wa Kata ya Nyambono,wilayani Butiama,mkoani Mara, wakasema uchaguzi uliofanywa katani humo umeshinikizwa na viongozi ili wasikose kura kutoka kila kijiji katika uchaguzi wa 2014 wa serikali za Mitaa.
Mahali pengine uchaguzi wa Mabaraza ya Katiba ulifuata itikadi,dini na ukoo kiasi kwamba watu makini walitupwa nje,wakachaguliwa watu ambao hata kujua kusoma ni taabu. Sasa hawa watapitia vipi Rasimu ya Katiba,ikiwa hata kuzungumza Kiswahili ni shida?
Ama Tume ya Jaji Warioba inataka kushirikisha wananchi wengi mbumbumbu sana,mradi tuseme Katiba Mpya ilitungwa na wananchi wa kawaida,hata kama hajui kusoma wala kuandika?
Hawa wajumbe wa Mabaraza ya Katiba, wengi wao hata Katiba hajui ni mnyama gani, na kwa kuwashawishi wananchi wenzao ili wawachague wamedhihirisha hawafai,maana ni wala rushwa ambao hawawezi kutuletea Katiba ya maana,isipokuwa mianya ya posho na ulaji!
Nawashangaa wananchi hasa wa vijijini na mitaa ya Mijini,kuhongwa chai,maharage na unga ili wawachague watu vipofu ili wakapitie Rasimu ya Katiba! Ati hii ndiyo Demokrasia(Participation of Majority?) ushirikishaji wa watu wengi mbumbumbu ili kututungia Katiba Mpya!
Nawashangaa wananchi,kuwachagua watu Mbumbumbu Mzungu wa Reli(si wote) ili kupitia Rasimu ya Katiba,kwa sababu tu walituhonga,ama walikuwa wa dini yetu,jamaa zetu ama wa chama chetu!
Nimewaona wanachama wa chama Fulani cha siasa wakimsuta Diwani kutoka chama chao kwamba walimsaidia kushinda sasa amewatupa kwenye ulaji wa Mabaraza ya Katiba ya Kata!
Nimewasikia wanachama wa chama kimoja wakilalamika kuachwa katika mabaraza hayo kwa kuwa walikuwa na itikadi tofauti!
Kwa nini Rasimu ya Katiba Mpya kujadiliwa na wajumbe waliopatikana kwa mizengwe na rushwa, wakati hata uelewa wao ni shida kubainika miongoni mwa jamii?
Eti jambo la msingi kama Katiba linatawaliwa na tama ya posho,udini,udugu,kujuana na itikadi za vyama-huu ni umajununi.
Bado hatujui umuhimu wa Katiba, ingawa vijijini inasemwa kuwa wananchi hunyanyaswa sana na polisi,watendaji wa vijiji na kata,hata Haki za Binadamu hukiukwa sana,badala yake wamechaguliwa watu kwa rushwa ili wakatazame Rasimu ya Katiba!
Hawa wapenda posho wataitazama Rasimu ya Katiba Mpya ili kutafuta Haki zao za Msingi kwenye Katiba Mpya, ama ni kichekesho?
SHeria Na 1(5) inatoa Uhuru wa Maoni(Freedom of Expression) lakini uhuru gani ikiwa wamechaguliwa mbumbumbu ili wakatetee raia wa vijijini kunyimwa malipo ya mazao yao na kuswekwa rumande na polisi na watendaji wa kata hadi wahonge mbuzi,ndipo wapewe dhamana?
Katiba ya kuwatoa kamasi miungu watu wa vijijini itatungwa na watu wasiojua kusoma na kuandika?
Kuna wasiwasi jumuiya za wakulima vijijini kuwakilishwa na watu wa ajabu sana,wakati jumuiya zingine kama wafanyakazi wakiwemo walimu na wale wa migodini wamewakilishwa vema na watu wenye weledi kuingiza mahitaji yao katika Katiba Mpya.
Hapa,demokrasia ambayo ni ushirikishwaji wa wengi imekosa shabaha kuwaleta watu wenye nia ya kugombea posho kupitia Rasimu ya Katiba!
Posho na Katiba ni vitu viwili tofauti,na namwomba Jaji Waryoba kuwahoji watu hawa mlangoni kabla ya kushiriki mikutano hiyo kwa kulala usingizi na kusubiri kusaini posho nono inayotegemewa kutoka Tume ya Katiba.
Nashauri zoezi hili lisitishwe,ili wakulima wajipatie wawakilishi wenye weledi ili kutetea Haki za Wakulima vijijini ambao ni wengi lakini hawana hospitali wala barabara,licha ya Pato la Taifa kutokana na Kilimo wanaolima wameachwa nyuma wakati miundo mbinu inapojengwa mijini.
Bei za mazao zinaporomoka wakati wafanyakazi wa mijini wanapoongezewa mishahara mikubwa, wanalalama sana wakati mkulima anapohongwa chai ili amchague mbumbumbu kwenda kuandika Katiba!
Demokrasia haina maana ikiwa itawashirikisha watu wa ajabu sana kupitia Rasimu ya Katiba,utungwe mtihani watakaoshinda wapitishwe kwenda kupitia Rasimu hiyo ya Katiba ambayo ni muhimu kwa Tanzania ya kesho,lengo ni kuwatimua wajumbe wapenda posho katika mikutano hiyo.
0786  324 074
www.congesmrambatoday.blogspot.com

No comments:

Post a Comment