Monday, August 5, 2013

nduli Amin Dada(4)



                                    
Na Conges Mramba
Baada ya Amin kuingia madarakani, watu wa kabila la Lango na Acholi la Milton Apollo Obote,waliuliwa kwa maelfu, na maiti zao zikaliwa na mamba wa Mto Nile huko Jinja.
Wahindi wakatimliwa mwaka 1972 maduka yao wakapewa rafiki za Amin mjini Kampala,ndiyo maana hata leo kuna watu wanampenda Amin kuliko Museveni.
Naam,tumejadili Operation Thunderbolt, iliyomtoa jasho Amin kushabikia wateka nyara wa Kipalestina,huku akakosana na Israeli na Magharibi.
Kile kikosi cha makomandoo wa Israeli kilienda zake salama,kikapokelewa kwa heshima kubwa.Yule Jonathan komandoo aliyeuliwa alizikwa kwa heshima kubwa kama shujaa wa taifa.
Utawala wa Amin wa miaka minane ukaandamwa na mikosi hadi raia wake wakaanza kumwasi nao ni akina Museveni,Tito Okello na wengine kama tulivyoona katika toleo lililopita.
Amin alikosana siyo na Nyerere tu,bali hata Rais Moi wa Kenya zama hizo,akitishia kwamba hata Maili 20 Nairobi ilikuwa sehemu ya Uganda tangu zama za ukoloni.
Tumeona Amin akitimliwa mamlakani na kufia huko Saudi Arabia,baada ya Museveni kukataa azikwe Uganda.
Hata hivyo,mwanaye Amin,Jaffar siku za karibuni alifanya jambo la kuondoa chuki na kudumisha urafiki.
  Aprili, mwaka 2009, ni mwezi ambao kulitokea vitu vingi adhimu sana, na vya kukumbukwa sana hapa nchini.
      Safari ya mwana wa Dikteta wa zamani wa Uganda , Jaffar Amin(47) aliyesafiri kutoka Uganda hadi Mwitongo, Butiama, mkoani Mara.
    Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza, BBC, iliratibu safari hiyo ya Jaffar, ambaye ni mtoto wa nne, kati ya watoto takriban 60 wa Amin.
 Jaffar alikutana na mtoto wa Pili wa Mwalimu, Madaraka Nyerere.
   Ziara ya Jaffar huko Mwitongo, Butiama katika mwezi huo wa Aprili, mwaka 2009, inatukumbusha miaka 34 kamili baada ya kuanguka kwa utawala wa baba yake huko Uganda , Aprili 11 mwaka 1979.
   Amin Dada, alitimuliwa na majeshi ya Tanzania mwishoni mwa vile vita vya Kagera; akatimkia Sudan, Libya kisha Saudi Arabia, alikofariki dunia mnamo Agosti 16 mwaka 2003.
   Naam. Ziara ya Jaffar Amin huko Mwitongo, Butiama mkoani Mara, ilikuja wakati wa Kumbukumbu ya 87 ya kuzaliwa kwa Mwalimu mahali hapo.
 Nyerere alizaliwa Aprili 13 mwaka 1922.
   Tena, Jaffar amekuja Tanzania wakati hayati Mwalimu alipojadiliwa sana katika lile Tamasha lake lililowaleta nchini wasomi na wanazuoni maarufu Afrika; kama Prof. Wole Soyinka wa Nigeria .
   Tumjadili kidiogo Jaffar Amin, ambaye leo ni kiongozi wa familia ya Marehemu baba yake, Idi Amin Dada, mtawala wa zamani wa Uganda (1971-79).
   Mwaka 2005, alikwenda Akokoro, ili kuhudhuria mazishi ya Dk. Apollo Milton Obote. Amin ndiye aliyempindua Obote mwaka 1971 alipokuwa nchini Singapore akihudhuria Mkutano wa Jumuiya ya Madola(Commonwealth); Obote akakimbilia Tanzania .
   Kitendo cha Jaffar kuhudhuria mazishi ya Dk. Milton Obote, hasimu mkubwa wa baba yake, kilivuta hisia za watu  wengi, hata kuona msamaha na maridhiano miongoni wa Waganda na Waafrika wengine wa zama zetu hizi.
 Jaffar Amin, ni somo kwa Waafrika wote zama hizi, kusameheana na kuacha chuki na vita visivyo na sababu, wakatiti sisi Waafrika ni ndugu wamoja.
  Jaffar, alipowapa pole familia ya Obote katika msiba huo, akageuza upya historia na kuanza kumuumba upya babaye, Dikteta wa zamani wa Uganda, aliyejibandika vyeo lukuki  kama, Field Marshal, Mshindi wa Dola ya Kiingereza, Mwanamasumbwi Nguli Duniani, Bingwa wa Kuogelea na mwenye Medali za kutukuka sana kama Victoria Cross n.k!
   Jaffar, anapofika Butiama kuzungumza na Madaraka Nyerere kwa msaada wa Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya BBC, Bwana Solomon Mugela, anawaondoa Watanzania katika lindi la fikra hasi za kumtazama Amin kama ‘Joka Kuu’ la kale la Uganda, Nduli, muuaji, mla nyama za watu, hususan adui zake wa kisiasa.
 Nazungumza umuhimu wa toba na msamaha kwa sisi Waafrika, yaani kuachana na uhasama ili kutafuta umoja na mshikamano kisha maendeleo yetu na wanetu.
  Amin, alishatengenezewa filamu tatu zenye kuonyesha enzi ama zama za utawala wake wa kikatili na kimabavu sana kulinganisha na ugaidi wa siku hizi.
    Sauti ya Nyikani  hupenda sana kuzitazama zifuatazo:
The Rise and Fall of Idi Amin Dada, na ile ya Forest Whitaker, iitwayo, The Last King of Scotland.
  Katika sinema hizo, Amin huonyeshwa kama mtawala katili sana , pumbavu, zuzu, mpenda anasa na  mpenda wanawake, anayetawala nchi kwa hofu na vitisho karibia kumuua kila anayemuota ndotoni, akimpinga, akimsaliti hata kumchukulia mmoja wa wakeze.
   Filamu nyingine iitwayo, 90 Minutes at Entebbe au The Entebbe Raid, inatukumbusha Uganda ilivyoanza kuvunjika vipande, baada ya Bwanamkubwa Amin kuvuruga uhusiano wa kidiplomasia na Wazungu.
   Amin, alijiweka upande wa Waarabu hususan Wapalestina, magwiji wa medani za ugaidi wa kuteka  nyara ndege, kama hiyo ya Air France Air Bus, iliyokuwa safarini kutoka Paris,Ufaransa, kwenda Israeli, ikatekwa na kupelekwa Entebbe.
  Naam, tunamjadili kidogo Marehemu Idi Amin Dada na mwanaye, Jaffar Amin aliyefika Mwitongo, Butiama mwaka jana, kuja kumuenzi Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu, miaka 30 baada ya Vita vya Kagera, vilivyomwondoa madarakani, Uganda, Marehemu babaye, 'Joka Kuu' Nduli Amin, aliyelala mauti kaburini Saudi Arabia.
    Nataka kusema kwamba, namkumbuka Amin kwa ‘kuwachachafya’ vilivyo Wazunguna magabacholi.
 Naam, wakoloni ambao leo hutetemekewa sana kwa kicho utadhani miungu; hupigiwa goti na kulambwa dole gumba na watawala wetu waliojigeuza manyampala wa Wazungu.
   Watawala wa Afrika waliojaribu kuwapinga Wazungu ni Nelson Rolihlahla Mandela tu; labda na “R.G” Mugabe  na Kanali Muammar al-Qaddafi, tena kwa sababu zao!
 Nani leo atathubutu kuwapinga wazungu?
     Waama, filamu iitwayo, The Rise and Fall of Idi Amin Dada, inatukumbusha  baadhi ya vituko vya Amin ambavyo kwa kiasi kikubwa sana hushadidia ukombozi wa mtu Mweusi dhidi ya Weupe.
    Siku ile Mkutano wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika(OAU kabla ya kuwa AU), ulipofanyika mjini Kampala , Amin alibebwa na Wazungu katika machela, alipokuwa akiingia kufungua mkutano!
   Viongozi wenzake waliokuwa tayari katika chumba cha mkutano wakashangaa kuona Amin anaingia kwa staili ya kubebwa na Wazungu katika machela.
  Kumbuka msomaji wa safu hii, zama za Ukoloni ni Waafrika waliowabeba wakoloni wa Kizungu katika machela.
 Mwandishi, rafiki yangu, Prudence Karugendo, aliyekuwa Kampala zama hizo, ananiambia kitendo hiki hakijawahi kufanywa,bali propaganda za Magaharibi tu.
   Pia, wakati fulani, Amin alimhukumu kifo Mhadhiri wa Kiingereza, Dennis Hills , kwa makosa ya kuwasumbua na kuwanyang’anya ardhi wanakijiji.
 Jumuiya ya Kimataifa ilipomzonga sana Amin ili kumwacha huru Bwana Hills, akasema kwamba  hadi kama  Waziri Mkuu wa Uingereza, James Callaghan, angeruka kutoka London hadi Kampala, kuja kupiga goti na kumwombea msamaha Hills, ndipo angeondolewa kitanzi kilichomkabili!
 Siku hizi, hapa Afrika  iko mahakama yenye uwezo wa kumuhukumu Mzungu hata mwizi,gaidi, na mbakaji, bila kuuliza alikotoka,kama wamfunge jela au wamwachilie 'Fasta'?
 Hapa Tanzania, kasisi mmoja wa Katoliki,toka Italia alibaka wanafunzi wa kidato cha tatu jijini Mwanza, akafikishwa mahakamani na kuamuriwa kuondoka nchini, asije akaswekwa  'mangenge' hapa,akanyea mtondoo wa Butimba!
   Hiki ndicho kilikuwa ‘kidume’ cha Bwana Mkubwa Amin dhidi ya Wazungu.Aliwatoa kamasi Wazungu na Wahindi,bila kicho,kwa maslahi ya Waganda!
 Amin, alikuwa na ubavu wa kuwatoa kamasi Wazungu, bila kuwaogopa Malkia Elizabeth II, Waziri Mkuu wa Uingereza,wala nani!
Aliwatimua Waasia 100,000 mwaka 1972, biashara zao walizoacha nyuma akawapa Waganda wa kawaida sana , ili nao wapate kukabiliana na machungu ya maisha!
Walikuwa na hati za kusafiria za Uingereza,wakati wanafanya biashara Kampala! Walihamisha utajiri wa Uganda hadi Ulaya kwa utulivu mno, hadi Amin alipokuja kuwatolea uvivu.
    Leo, hata hapa Tanzania kuna Waasia wenye uraia na Hati za Kusafiria za Uingereza , Canada na Marekani, wanaofanya biashara za magendo, ya fedha chafu, utapeli,ufisadi na wizi na uhujumu uchumi, bila kusahau ufisadi wa EPA,rada kanyaboya ya BAE Systems, lakini viongozi wetu huwakodolea macho pasipo kuwachukulia hatua kali,  kama  Bwana Mkubwa, Amin!
 Namkumbuka Mhindi, Shailesh Vithlani alivyoiingiza 'mjini' Tanzania kwa rada kanyaboya kutoka BAE systems!
 Rada ya fedha ndogo, wao wakala 'cha juu' hadi zikafika Dola za Marekani 40,000!!
    Nikipembua uhalifu na unyama wa Amin, hasa aliofanya dhidi ya raia kwa kutumia polisi wa siri waitwao, The State Research Bureau, nasisitiza wasomaji wa safu hii  adhimu na viongozi wazalendo wasiache kumuiga Amin kwa vitendo vya kimapinduzi alivyofanya (hata kwa bahati) ili kuwakomboa wanyonge.
   Nazungumzia vitendo vya kihalifu alivyokataa Amin, hata kama walifanya Waingereza.
  Waingereza wanatupa sisi Tanzania misaada.
Kila mwaka hiyo misaada huongezeka.
Mwaka 2003/2004 iliongezeka kutoka pauni milioni 80(sh. Bilioni 208) hadi pauni milioni 110(sh. Bilioni286) mwaka 2006 na 2007.Asilimia 70 ya misaada ya Uingereza huingia katika Bajeti ya serikali.
   Ni kwa sababu hii, mashirika ya misaada ya Uingereza na Bunge huwa na sauti kubwa sana hapa kwetu hadi kuingilia ‘mambo ya jikoni’ kwa maslahi ya Uingereza.
Haya ndiyo Amin aliyokataa enzi zake.Hata leo viongozi wetu wakimuiga Amin, kuna ubaya gani,na kwa maslahi ya umma?
 Nahitimisha safu hii  leo, kwa kuwakumbuka Waingereza vijana wawili:
 Nigel David(23) na Brett Richard(20) waliotiwa mbaroni kwa tuhuma za kumbaka kisha kumuua msichana kigori wa Kitanzania, Conjesta Ulikaye, mnamo Novemba 10, mwaka 2004.
   Tukio hilo lilitokea katika ufukwe wa Bahari ya Hindi, katika hoteli ya Silver Sands, Dar es salaam .
   Shauri la kesi ya mauaji likashughulikiwa kwa siku 36 tu, Nigel na Brett wakafikishwa mahakamani ‘Fasta’ Novemba 16; yaani siku sita tu baada ya tukio.
  Vibaka wa hapa wanasota rumande hata miezi sita bila upelelezi kukamilika!
Ndiyo maana kila siku hugoma kushuka kwenye karandinga na kujipaka kinyesi, hadi serikali iwajali kama inavyowanyenyekea Wazungu, naam na wenye cheo.
   Kesi hiyo ilifutwa Desemba 22 mwaka huohuo kwa mujibu wa kifungu 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 1985.
   Safu hii, iliwahi kumuuliza Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), Geofrey Shaidi wakati huo(sasa Jaji), Machi Mosi mwaka 2005 alipokuwa jijini Mwanza:
    Hao Waingereza wawili(walikuwa wanajeshi wa nchi hiyo waliokuwa mapumzikoni Dar, wakitokea vitani (Irak) waliachwa huru kwa maslahi ya umma wa Tanzania, au maslahi ya Uingereza?
    “Hawakuachwa huru kwa maslahi ya Uingereza au ya Tanzania …ushahidi uliokuwepo haukutosha!
Wasingeendelea kung’ang’aniwa bila ushahidi,” DPP Shaidi alisema.
   “Hata hivyo, kesi(dhidi ya raia) hazicheleweshwi na ofisi ya DPP, zinacheleweshwa mahakamani, zinaposubiri kupangiwa tarehe ya kusikilizwa.
Hivyo, faili la Wazungu lilipofika kwetu, tukalishughulikia(fasta?) kama kawaida”,
  alifafanua DPP Shaidi wakati huo, huku akikanusha madai kwamba Waingereza hao hawakuachwa huru kwa sababu ya kuchelea kunyimwa misaada na Uingereza endapo wangehukumiwa kutiwa kitanzi.
    Laiti Nigel David na Brett Richard wangefanya unyama wao huo wa kumbaka msichana kwa zamu na kumsababishia kifo huko Uganda , enzi za Amin, bila shaka wasingeepuka kitanzi!
   Hata kama Mawaziri Wakuu kama Margaret Thatcher, James Callaghan, Edward Health, John Major, Tony Blair na Gordon Brown, na David Cameron  kwa pamoja wangemkoromea Amin, bila shaka Nigel na Brett wangenyongwa tu hapa hapa Dar es salaam!
  Unacheza na Amin?
    Hata hivyo, hongera BBC  mwaka 2009, kutukumbusha mikasa ya lile Joka Kuu, “shujaa” Nduli Idi Amin Dada!!
   Ziara ya Jaffar imetukumbusha kuyasema pia mazuri ya marehemu, wakati huu tunapoingia mwaka mpya,ili tujirekebishe.
Tulizowea kumsema Amin kwa mabaya tu.Kwa heshima ya Jaffar, shime tutazame upande wa pili wa shilingi.
 Baniani mbaya,kiatu chake dawa, nikitazama viongozi wetu siku hizi wanavyowanyekea Wazungu na kuingia mikataba mibovu na wageni, wakiwemo matapeli wa Kihindi, kama Vithlani, nikikumbuka EPA,Dowans, Richmond na uchafu mwingi...namkumbuka Nduli Idi Amin, kwamba ingekuwa zama zake, lazima angewatoa kamasi hawa    magabacholi.
 Naam,  kwa sababu hiyo tu....nampenda 'Joka Kuu' Nduli Idi Amin Dada!!
     Congesdaima@yahoo.com
      0786/0754-324 074
  
   


No comments:

Post a Comment