Wednesday, August 1, 2012

mbio, kutoka kwa Shetani ili kuomba hifadhi ya ukimbizi kwa Luciferi

     
ARISTOTLE (384-322 BC) ni miongoni mwa wanafalsafa wa Ugiriki, ambaye wakati wa uahai wake aliwahi kusema hivi:
“To say of what is not, or of what is not that it is-is FALSE. While, to say what of what is that it is and of what is not that is not, is TRUE!!”
Falsafa ngumu hii ya Aristotle nimeitafsiri hivi:
 “Kusema namna kitu ama jambo lisivyokuwa ni UONGO,wakati kusema namna jambo au kitu kisivyokuwa wakati kweli hakiko hivyo,huu ni UKWELI”.
Naam.Ukweli unaweza kuongopa,pindi nusu ukweli unaposimuliwa au kuzungumzwa,kwa nia ya kuongoza watu kwenye UONGO.
UKWELI ni nini basi?
Kulingana na wanafalsafa, Ukweli ni mwafaka baina ya matukio na uhalisia wa mambo(Truth is Agreement with Facts and Reality).
Aghalabu,natamani kuwa mkweli siku zote, ili nisimulie matukio yaliyowahi kutukia duniani kama mifano hai ya uhalisia wa mambo,kwa lengo la kuwaongoza wasomaji wangu wote katika ukweli.
Kwa mfano: Nisemapo, “Amara Kanu Nwanko ni mke wa mwanandinga nguli wa Nigeria,Nwanko Kanu”, nasema Ukweli.
Pia nikisema Barack Obama wa Marekani, ni    Rais wa Marekani ambaye hana maslahi yake hapa Afrika, na Mwafrika kumshangilia sana na kumtegemea ni kupoteza muda wake bure, nasema ukweli mchungu.
 Tuukubali ukweli,ili utuweke huru-ukweli huwaweka watu huru kweli kweli.
Sasa, niseme kwamba Tanzania kuna magaidi wa mafanikio yao wenyewe. Kila mtu gaidi wa mafanikio yake, aghalabu ni yeye mwenyewe na wanaomzunguka.
Nimekuwa nikiandika harakati za magaidi,kwamba siyo majambazi wa kawaida ama majangangili wanaofanya uhalifu kwa nia ya kujipatia chumo la faida.
Magaidi wa sura ama mtazamo sawa na wanaharakati wa Haki(za Binadamu?)wanapopigania mambo yao na maslahi yao.
Kama vile magaidi wa kawaida, kupigania haki kwa njia hii,ni lazima kupora haki za wengine. Kujitoa mhanga na kupoteza maisha maana yake ni kupoteza haki ya kuishi kwa nia ya kuwaangaza wengine.
 Neno ‘mhanga’ ama ‘wahanga’ halimaanishi watu waliopatwa na ajali kama ya Mv.Skagit huko Zanzibar. Hakuna wahanga wa Mv.Skagit hata kidogo, bali kuna waathirika wa ajali ya meli,basi ama ndege.
 Kujitoa mhanga, ni kuwa hiari kufa kwa ajli ya jambo Fulani(harakati) na wala hakuna watu wanaojitoa(wanaopenda) kufa ajalini. Waandishi wa habari wameuwa wakiongea Kiswahili kibovu sana kwamba ‘wahanga’ wa ajali!
Wanaharakati,hususan magaidi hujitoa mhanga,huwa radhi kupoteza maisha yao na ya  wengine ili kupigania maslahi Fulani.
Hii siyo haki aslani. Ni nusu haki na nusu dhuluma. Nusu haki na nusu dhuluma haiwezi kuwa haki, na haiwezi kuwa kweli. Twende na msingi huu.
Tanzania kuna harakati za kigaidi zilizoanza zamani sana; kwa kile kiitwacho harakati za UKOMBOZI dhidi ya UTUMWA Mamboleo,ukoloni ama mfumo kandamizi.
Kuna ufisadi,ubwenyenye,ubeberu,pasipo uhuru ama usawa n.k
Feburuari 26, mwaka 1982,Ndege ya Boeing 737 ya Shirika la Ndege Tanzania, “Tango Charlie 207” iliyokuwa na Jina, ‘Kilimanjaro’ mbavuni, ilitekwa na magaidi wa ki-Tanzania.
Waliilazimisha kwenda London. Ilikuwa na abiria 74 na wafanyakazi watano,na ilitokea katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza na ilitaka kusafiri hadi Dar es salaam, magaidi hao walipotokea na kuiteka nyara,wakailazimisha kwenda London!
Iliendeshwa na Kapteni Deo Mazula,wakati huo wakati mimi nikiwa kijana mdgogo,nikipenda sana kusoma hadithi za Upelelezi,hususan za wateka nyara wa Kipalestina,na makomandoo wengine mahsusi.
Nimeandika sana juu ya ndege ya Ufaransa, Air France Air Bus, iliyotekwa nyara na kulazimishwa kuja kutoa Entebbe,Uganda,mwaka 1976. Zilikuwa harakati za kudai haki,lakini haki hizi ziliondoka na maisha(haki ya kuishi) ya watu wengine wasio na hatia-Hii aslani siyo haki na si KWELI. Tuendelee na msingi huu kwamba,nusu haki na nusu ukweli siyo ukweli.
Turejee kwa wateka nyara wa ki -Tanzania mwaka 1982.
Yassin Membar(21),Mohammed Tahir(21),Abdallah Ali Abdallah(22),Mohammed Ally Abdallah(26) na kiongozi wao Musa Membar(26) waliteka ndege hiyo ya ATC kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza, wakailazimisha kwenda London, Uingereza.
Lilikuwa jambo la tashtiti.Walikuwa na silaha mwanasesere.Walikuwa magaidi wanagenzi.
Usalama dhalili katika uwanja wa ndege wa Mwanza uliwawezesha kuingia ndegeni na midoli ya bastola na kuwatisha abiria,rubani na wafanyakazi wa ndege hiyo.
Uwanja wa ndege wa Mwanza, umeendelea kuwa dhaifu kiulinzi hadi miaka ya karibuni, mtunzi wa Filamu ya Mapanki, The Darwin’s Night Mare, Hubert Sauper  alipoingia na kamera katika chumba cha kuongozea ndege na kuanza kupiga picha nyuki wakiranda katika vioo vya dirisha,kisha alipiga picha maeneo ya kijeshi, jambo ambalo lilikuwa hatari mno kwa usalama wa nchi.
Sauper,ni raia wa Australia aishiye Ufaransa, na alisema mwenyewe kwamba alifanikiwa kupiga picha hapa kwa sababu aliwapa wahusika rushwa ili afanikishe Documentary yake iliyompa tuzo ya Oscar.
Naam. Wale jamaa, akina Musa Membar, waliwateka nyara abiria,wakaikagua ndege na kupata bastola halisi tena ‘revolver’ iliyokuwa katika chumba cha rubani.
Walipata bastola nyingine yenye risasi baada ya kuwapekua abiria.
Tena, walinyakua Shotgun mbili zilizokuwa na risasi ambazo zilikuwa mali ya abiria, zilihifadhiwa kizembe-Hivyo safari ya London ikakolea bila wasiwasi.
Kwa kifupi, ndege hiyo ilikwenda London,na ilikuja kurejeshwa na abiria wake 74 Machi 4, mwaka huo wa 1982, wakapokelewa kishujaa sana Dar es salaam, nakumbuka Radio Tanzania Dar es salaam ilitangaza ‘Live’ marejeo ya ndege hiyo.
‘Magaidi’ hao walifungwa London kati ya miaka mitatu na minne kwa  makosa ya ugaidi,hata kama walikuwa na madai mazuri nitakayoeleza punde. Ilikuwa  kumkimbia Shetani na kutafuta hifadhi ya ukimbizi kwa      Ibilisi!
Sababu za akina Membar kuteka nyara ndege,ni maisha magumu,ukosefu wa ajira hususan kwa vijana kama wa zama hizi, umangimeza wa utawala wa  Hayati Mwalimu Nyerere, na rushwa  kama ufisadi  wa siku hizi. Tabia ya mtu kuharibu hapa na kuhamishiwa kwingine haikuanza leo.
 Kumbuka, Mwalimu hakutawala kama zama hizi za ‘domo kaya’ tunazoita za “Freedom of Expression” zama hizo Usalama wa Taifa waliogopwa kama radi! Siku hizi mnawatukana hata baa,zamani walihesabu vizibo vya bia!
Zama hizi ndizo Marehemu Rammadhan Ongala ‘Remmy’ aliimba kwamba fundi viatu alipewa kuwa Mkuu wa FAT unakumbuka, msomaji?
Nataka kusema kwamba, hao akina Membar wangeteka nyara ndege leo na kwenda London kusema maisha ni magumu sana na hali ni mbaya ndiyo maana wamechukua uamuzi huo-WANGESHANGILIWA SANA!
Wangeonekana wanaharakati,mashujaa,wanamapinduzi, walioandamana kueleza hisia zao!
Wanamapinduzi huwa na imani thabiti juu ya mabadiliko ya kisiasa,kijamii na kiuchumi; hudai kufanya harakati kwa maslahi ya jamii nzima. Hawa wa        kwetu hapa,ni domo kaya tu.
Siku hizi,huwa nasikia watu wengi vijiweni wakisema Hayati Mwalimu Nyerere alikuwa Rais mzuri sana, kama malaika!
Huwa nacheka sana!
Nakumbuka akina Kapteni Tamimu, Uncle Tom, na wenzao waliposema walilazimika kutaka kuipindua serikali,kwa sababu ya hali mbaya,upendeleo,rushwa,maisha mabaya,magumu hata wanajeshi kuvaa viraka!!
 Najua,baada ya vita vya Kagera(Novemba 1978-Aprili 1979) nchi ilitumia takriban Dola za Marekani milioni 500 kwa gharama za kumtia adamu na kumpindua Nduli Idi Amin.
Askari wetu 620 walipoteza maisha katika vita hivyo, nchi ikafilisika,bidhaa madukani zikapotea,watu tukavaa matairi ya magari miguuni!
Nataka kusema kwamba, hali mbaya ya uchumi haikuanza jana hapa nchini.
Tumetumia majani ya mipapai kufua nguo,tumewahi kuunga majivu badala ya chumvi sisi, wakati huo vijana wadogo.Ingekuwa hivyo leo mngeandamana sana.
 Kwa nini akina Membar na akina Uncle Thom hawakushangiliwa kwa ‘ugaidi’ wao zama hizo?
Hazikuwa zama za haya ya sasa, siyo kwamba watu walikuwa wajinga.Walikuwa wastahimilivu,wazalendo tena wasikivu na wachapakazi.
Kwanini wananchi walichanga ng’ombe,mbuzi na udaga wao kugharimia vita ya Kagera ? Hawa wapenda raha na walalamikaji wangechanga nini? Hata kama wangechangia vita, michango ingeporwa hata kabla ya kufika Mstari wa Mbele, hawa huibia hata majeruhi na marehemu wa ajali hata ya Meli ya Mv. Bukoba! Utajiri wa Damu!
Hakika sisi Watanzania hamnazo! Leo,tunasikia watu wakisema eti tupigane sisi kwa sisi mafisadi wametamalaki! Uzuzu!
Eti tumekuwa na amani saana, sasa yatoshaa!! Eti ili nchi iendelee lazima vije vita kwanza. Kweli tumechoka na amani, ama utulivu tunataka vita? Vita mwavijua vizuri nyie?.
Siyo kwamba tunataka mapinduzi ya fikra na mitazamo ya wizi wizi tu na ‘shortcut’ na deal ambazo ni za wizi?
Hata hivyo,kila kiongozi huwa bora baada tu ya zama zake kupita.
Nyerere sasa ni bora maana zama zake zimepita. Alipokuwepo nimesema watu walitaka kumuua Jumapili moja Kanisani nadhani Mtakatifu Joseph,Dar. alipokwenda kuabudu, na wengine ndiyo hao walioteka nyara ndege,ili watafute ukimbizi London, wakaishia kolokoloni.
 Walisema, Nyerere alitawala kimabavu,kidikteta,kimangimeza n.k.Walitamani aondolewe, hakuondoka-siku hizi anakaribia kuitwa Mtakatifu Nyerere! Watu Bwana!!
Walimbatiza jina la ‘Nabii Musa’kwamba miezi ile baada ya vita ilifananishwa na safari ya Waisraeli kutoka Misri kwenda Kanani.
Akina Membar walipofika London walijidai kutumwa na Abdulrahman Mohamed Babu aliyekuwa Mkimbizi wa kisiasa na alirejea nchini wakati wa vyama vingi,miaka ya 90.
Ukweli kwa mujibu wa Aristotle, ni kwamba hata wakati wa Nyerere kulikuwa na shida kama hii ya sasa.
Watu wajinga walidhani mapinduzi ya umwagaji damu ama ugaidi ilikuwa ndiyo suluhu ya matatizo,kumbe wapi bwana!
Leo,tunasikia mambo ya kutisha,utadhani hakuna kinachoendelea. Tunaona watu wanakasirika,migomo,maandamano,watu wanapigwa risasi na mabomu ya machozi.
Akina Dakta Ulimboka sasa wanatekwa nyara kama zama zile za akina Membar kuteka nyara ndege n.k Kuna machafuko na madai ya haki kama zama zile. Lakini namna ya kutafuta suluhu ni tofauti sana ni ‘Violence’ badala ya kile alichosema Mpigania Haki za Weusi Marekani, Martin Luther King Jr. “Nonviolence Resistance”.

Nimetumia ‘Facts’ ili kusema ukweli kwamba hakuna wakati watu walipokuwa hawalalamiki hapa duniani,siyo hapa nchini tu. Hata Marekani, Wall Street ,kuna  maandamano, Uingereza kuna migomo hata sasa wakati wa Olimpiki. Mbinguni,kuliwahi kuwa na maandamano na mgomo,Lusifa akamgoma Mungu,muumbaji wake, Soma Ufunuo 12.
Nataka niwaambie Watanzania, hali mbaya na wakati mgumu wa uchumi vipo mara zote tangu zamani,na tuendako mbali na kuvumbua mafuta,gesi na robot,hali itakuwa mbaya sana.
Mara zote, wanaharakati huamka kudai hali bora zaidi na maandamano hufanywa ili kudai haki zaidi,maendeleo zaidi-maendeleo hayana mwisho.Hii ni dhana ya mapinduzi watu kutafuta hali bora zaidi.
Sasa, tutafute hali hii bora kwa akili. Tusianze kupigana na kuuana kwa kisingizio cha uchumi mbaya na rushwa miongozi mwetu.
Juzi, nilikwenda kwa Afisa Uhusiano wa Mamlaka ya Maji Jijini Mwanza,MWAUWASA,Robert Masunya, nikamwambia,
“Sisi hatuna maji ya bomba sasa ni karibu siku nne,watu wanatumia maji machafu,kwa nini?”
“Mimi nakwenda msibani, hilo gari hapo linaningoja mimi”, alisema huku akinionesha hilo gari linalomngoja.
“Hiyo habari ya msiba unaokwenda ndiyo jibu la matatizo yetu ya kukosa maji Mwanza,hadi akina mama wanaamka saa 9 usiku kwa mwezi mzima?” nilimuuliza.
“Sasa wewe unanilazimisha niseme nini? Una kitu (mali)gani wewe?” alisema. Looh,nilishangaa.
Yaani huyu ananiuliza mimi nina nini,yaani masikini kwa kuwa nimeuliza ukosefu wa maji kwa siku nne mfululizo?” Nilijihoji. Hayo ya mali yalikujaje?
Huyu, siyo serikali. Ni miongoni mwa jamii yetu hii isiyojali shida za wananchi. Kaajiriwa katika taasisi ya umma, lakini wajibu wake hajui.  Hajui kuwa hajui.
Anaona mambo binafsi{kafa mtu mmoja) ni bora hata wafe milioni kwa kipindupindu kutokana na kunywa maji ya vinyesi huko visimani!
Sasa, tukipigana vita ndiyo tutawaondoa akina Masunya? La hasha.
 Vita havijapata kuleta haki. Dawa ya moto si moto,ni maji. Inawezekana bomu la Atomiki huko Nagasaki na Hiroshima lilimaliza vita vya Pili mwaka 1945. Lakini, risasi moja hutosha kuifanya nchi Jehanam.
Irak kuna vita tangu mwaka 2003, matatizo yao yameondoka? Kawaulizeni Somalia ama Libya.
Nataka kusema kwamba, nusu ukweli siyo ukweli,tujifunze kutokana na historia, ili kujua ukweli na kinachoujia ulimwengu,kufuatia kulipa visasi.
Nawashauri watu kusema,kupinga dhulula mioyoni mwetu kwanza na katika familia zetu kwanza,kabla ya kunyoosha vidole kwa wenzetu. Karibu watu wengi ni mafisadi watarajiwa.wakipewa vyeo ni uporaji tu wa mali ya umma!  Hao wapiga kelele wa        Bungeni,Dodoma wawasikia?
Niliwahi kuandika katika gazeti la Rai kwamba, “Kawimbo     “Mafisadi” katamu,lakini waimbaji wake hunuka mithili ya kwapa la Ibilisi!
Wabunge karibu wote wanatuhumiwa kuwa mafisadi,mara TANESCO,IPTL,RICHMOND sijui EPA.
Shime tuanzie myoyoni mwetu wenyewe kupigana vita vya kupinga dhuluma. Vita hivi tuvipige kwa wema myoyoni mwetu, si baya kwa baya dhidi ya wenzetu. Tutafute haki kamili na si nusu haki,kwa maslahi ya taifa letu. Tumepungukiwa Upendo wa Agape. Agape ni nini?
Itaendelea
0786 324 074
www.congesdaima@yahoo.com





1 comment: