Monday, August 20, 2012

MBIO KUTOKA KWA SHETANI ILI KUTAFUTA HIFADHI YA UKIMBIZI KWA IBILISI?-4

         
MWANAMUZIKI, Roger Whittaker, ndiye aliyeimba wimbo kwamba tusiwatumaini wanasiasa katika kutanzua matatizo ya yetu.
Whittaker, aliimba kwamba wanasiasa wote duniani hufanana; wamepinda mithili ya ndizi katika chane.Wote wana rangi moja ya njano,na hushikiliwa pamoja.
Roger Whittaker aliimba hivi:
“Politicians are like a bunch of bananas. They hang together, they all are yellow, and there is not a straight one”.
Wimbo mtamu! Nampongeza Msemaji wa serikali ya Kenya, Alfred Mutua,kutukumbusha wimbo huu katika kitabu chake kizuri sana, HOW TO BE RICH IN AFRICA. Msiniulize mtakipata wapi?
Kwa bahati mbaya sana, Watanzania wengi hawapendi kujisomea; bali kudanganyana vijiweni. Hawa, ni rahisi sana kuingia mtegoni;kutumainia wanasiasa na wanaharakati wawatawale fikra zao,wakidhani pindi waingiapo mamlakani,basi umasikini wao na shida zao vimetoweka.
Huku,ni kupungukiwa uwezo wa kuona kwa jicho la tatu. Hakuna mwanasiasa hata mmoja anayeweza kuishi kulingana na maadili mema na sheria nyoofu, “Moral Law” kiasi mkwamba atakuwa mzalendo wa kupindukia hata kujitoa mhanga kujiteketeza mwenyewe ili kuwaangazia wengine kama mshumaa. Upendo huu,huitwa Agape ama Agapao,kwa Kigiriki.
Wako wanasiasa waliojaliwa mvuto wa pekee, “Charism” wana uwezo na nguvu fulani ya ushawishi katika kauli zao. Augustine Lyatonga Mrema, aliwahi kujaribu,na Askofu  Zachary Kakobe na zama za “Magabacholi” alikaribia kuwachochea vijana kuwafukuza Wahindi kwamba ni ‘wezi wakubwa’ wa uchumi wa Taifa.
Rais Jakaya Kikwete naye alikaribia kuwashawishi vijana kwamba yeye ndiye suluhisho la matatizo yao ya ajira. Dk.Wilbroad Slaa,naye siku hizi anajaribu kudhaniwa kwamba akiingia madarakani,basi dhiki za sasa zinatoweka mithili ya kiza wakati wa jua kuzuka.
Unaweza kusema Rais Barack Obama wa Marekani, au mwingine yeyote kama Michael Satta, ni jibu la shida za raia mahali fulani. Hakika, mtu “Charismatic” anaweza kuandaa hotuba safi yenye mvuto wa kufanya hadhira hata kuhamisha mlima,lakini utekelezaji wa njozi zake ama ndoto ni kitu kingine tofauti kabisa.
Ubinadamu,umekabiliwa na udhaifu na mapungufu ya kiasili,kasoro tele ambazo lazima zionekane. Ubinadamu hauwezi kufikia ‘standards’ viwango vya ubora vilivyowekwa kwa ndoto na maneno ya mdomoni tu.
Kama tulivyotazama katika mfululizo wa makala haya,ukweli unapopokelewa na nafsi ya mtu,basi huwekwa huru kweli kweli. Tuupende ukweli mkamilifu, tusipende kauli zenye kuchanganywa nusu ukweli na nusu uongo. Nusu ukweli na nusu uongo,ni UONGO MKUBWA wa hatari, na Ibilisi alimdanganya Hawa kwa staili hii hii.
Ukweli mkamilifu ndiyo maadili, “ETHICS” na ndiyo mfumo wa kanuni za kutuongoza kutambua baina ya haki na dhuluma,ukweli na uongo na kweli na makosa.
Waingereza wanasema hivi:
Ethics is a system of principles that guides your conduct and helps you to distinguish between right and wrong or in some cases between two wrongs”
Wanafalsafa wanasema,maadili ni kiwango bora cha mwenenendo mwema, kwa sababu maadili yaandikwapo vitabuni na kuachwa humo,pasipo kuathiri mwenendo na tabia ya mtu,ni maadili gani na yana faida gani? Maadili huandikwa moyoni na kamwe siyo vitabuni.
Watanzania,tuna maadili ya vitabuni na midomoni; aslani hakuna mwenye kuamini ukweli na maadili na kuyaweka moyoni ili kuongozwa nayo-hii ndiyo shida ya kusema mengi bila utekelezaji. Hatusemi na kutenda hivyo.
Dk, Shaka Ssali,katika kipindi chake cha STRAIGHT TALK AFRICA kinachorushwa na Voice of America kila Jumatano Usiku, hupenda kusema, “Walk the walk and talk the talk-walk the talk” akimaanisha kusema maneno na kuyaweka katika vitendo(saying and doing),ndiyo utekelezaji wa sera nzuri.
Kuwa na utashi wa kisiasa, “Political Will” ni kitu kimoja,na kutekeleza sera ama njozi ni jambo la pili muhimu sana. Hii ‘Pilitical Will” haimfanyi mwanasiasa mwenye mvuto wa pekee kama Dk.Slaa kutekeleza yote mazuri aliyonayo njozini.
 Ni sawa na kocha wa timu anavyofikiri na akaelekeza wachezaji wake, badala ya kufanya walivyoelekezwa kulinda lango na kushambulia adui,kumbe wametoa mwanya kwa adui kufunga kirahisi! Namaanisha kitu hiki.
Maoni siyo “Facts” UHALISIA WA MAMBO.
Sisi Wtanzania siku hizi kila mwota ndoto husema kwa kinywa kipana na watu wakafuata. Hujawahi kusikia mtu akikwambia kwamba kwakuwa una homa,basi ni Malaria?
Haya ni maoni, “Opinion” na si ukweli na uhalisia,kwa sababu anayejua ukweli, ”Facts” kwamba mgonjwa anaumwa ugonjwa fulani,siyo watu wa kijiweni. “Laymen” ni Daktari.
Bahati mbaya,nchi hii, hatujui ni yapi maoni ya mhariri,yapi maoni ya wasomaji,nini msimamo wa gazeti na habari ni ipi ambayo iko ‘balanced’.
Tukio kama madodoki, masponji-sifongo! Kila tunachokuta mezani  tunafyonza. Tunafyonza maji safi na taka-hakuna kuchambua mambo kwa kina! Ni ushabiki tu, ni bendera na upepo.
Biblia,katika kitabu cha Warumi 5:13 hutwambia kwamba, Amri 10 za Mungu ndiyo kanuni ile ya maadili ya unyoofu, ambayo wanaita ‘Principles” inayoleta ‘The standard Behavior” ndiyo kioo cha kutuonesha mazuri na mabaya. Soma Warumi 3:5-7.
 Kazi ya kanuni hizi ni kuhimiza tabia nzuri,siyo kutusafisha. Kuwa na kanuni hizi au kuzisoma ni kitu kimoja,kuzifuata ni jambo muhimu zaidi. Kuna maadili wamepewa viongozi,Je wayafuata? Kanuni au maadili kazi yake ni kudhihirisha wazi mahali kasoro na madoa yalipo.
“It makes the dirt spots stand out more clearly and shows many more of them than one is able to see with naked eye”.
Huwezi kuona makosa kwa macho matupu yasiyo na kioo ambacho ndiyo maadili ama kanuni hizi. Wasio na kanuni, ama sheria za Mungu ambazo ni maadili ya ukweli ni vipofu siyo? Je wewe unazishika AMRI ZA MUNGU? Kipofu! Hata mimi ni kipofu,kipofu akiwaongoza vipofu,huishia kutumbukia katika rima refu.
Kanuni,maadili,Amri 10 za Mungu,sheria mya Mungu ni kielelezo cha tabia njema,bora(THE STANDARD BEHAVIOUR” ndicho kioo cha kutuonesha makosa na makasoro yetu-matongotongo,na hutwambia tafsiri ya dhambi na makosa.
 “The law tells us what sin is”,NAWAANDIKIA wenye hekima. Makosa ni dhidi ya binadamu wenzetu,na dhambi mtu humtendea Mungu. Dhambi zote ni makosa,na siyo lazima makosa yote yawe dhambi.
Kila binadamu hutamani kutenda na kutendewa mema-haki,siyo makosa na dhambi. Lakini,yuko mmoja awezaye kutenda mema wakati wote,mara zote na siku zote?
Niliandika katika makala yaliyotangulia kwamba Mkuu wa wilaya ya Handeni,Tanga, ambaye wakati huo alikuwa Mhariri Mtendaji wa New Habari Corporation na Mhariri wa Jarida la Rai,Mhingo Rweyemamu, alipata kuandika kwamba,katika nafsi ya kila mtu kuna Mbweha wawili-Mweupe na Mweusi-wanashindana.
Kwamba nafsi ya mtu ni uwanja wa vita(Battle Field) baina ya mambo mema na mabaya. Hii ni Falsafa ya Paulo Mtume wa Yesu katika kitabu cha Warumi sura 7 na 8.Anasema, hata katika nafsi ya mtu mwema kama Dk.Slaa,kuna ubaya unaoshindana na wema.
Maadili ni zana,kifaa,’tool’ cha kutuonesha njia ya mafanikio ya jamii na taifa.Lakini,kila mtu huvutwa,aidha kutenda maadili au kinyume chake(soma Warumi 7:7, 18-21). Je,yupo mtu wa kutumainiwa na kuaminiwa kila akisemacho,na kukifuata  kama kondoo?
 Kila mtu anapaswa kuwa na akili zake mwenyewe. Akili za mwingine changanya na zako-usipende kuwa bendera,kufuata upepo!!
Lile tulisemalo hatulitendi,na tulitendalo huwa hatulisemi. Huu ni ubinadamu wenye udhaifu na kasoro za kiasili. Unawezaje kuwaamini wanasiasa wewe?
 Ni kwa sababu hii,Mwanamuziki Roger Whittaker akatuonya mapema,kwamba wanasiasa wote ni ndizi-wanarangi moja na wamepinda!
Maandamano na migomo kila mahali duniani ni ushahidi kwamba kuna makengeza katika kila mambo ya mwanadamu.Utamwamini?
Kuna uasi,manung’uniko,malalamiko kila mahali sembuse serikalini?Serikali za wanadamu hulalamikiwa,hata serikali ya Mungu imelalamikiwa duniani,hadi Mircea akafungua kesi mahakamani.
Kama huu ndiyo ukweli,vipi kuhusu ‘a civic leader’ mwanasiasa wako, aiwe Jakaya Kikwete,Prof.Lipumba, Dk.Slaa,Mrema ama Obama?
Ni kwa sababu hii,Rais Kikwete alipotoa ahadi ya MAISHA BORA KWA KILA MTAZANANIA alikuwa akitoa njozi yake tu(maoni) na wala haikuwa  ‘facts’. Bahati mbaya kila ahadi tunaiamini hadi kukaribia kujitoa mhanga,ndiyo maana isipotekekezwa tunakasirika! Tunataka kupambana-vita!
Hizi kauli mbiu huwa shime tu ili watu wajitahidi kidogo. Tuwe na maadili mema tutajua wapi tulipokosea. Haya maadili ni suala mtambuka. Hayatuambii kupigana na serikali, “civil authorities” hata kama ikigeuka ‘The Most Oppressive regimes in history”. Huu ni ukweli mchungu,Tazama Warumi 13:1-7
Namtazama Martin Luther King Jr. Mpigania HAKI za Weusi wa Marekani. Alihimiza Wamarekani Weusi kutafuta haki zao,alikataza matumizi ya maasi na ghasia katika kufanya hivyo, NONVIOLENT RESISTANCE.
Wamarekani weusi walikandamizwa mithili ya Waisraeli huko Misri ya Faraoh.Walichinjiwa hata waoto wao wa kiume,walijenga ma Piramidi ambayo sasa yanadumu kwa karne nne. Ni moja ya maajabu saba ya dunia.
Wamarekani weusi walkandamizwa kila Nyanja,walibaguliwa.Martin Luther King Jr. alisema,kupambana na watesaji wako kwa njia ya maasi na vurugu, “Unjust system” ni sawa na kuungana na mfumo dhalimu huo.Udhalimu dhidi ya udhalimu.
Ninapokariri maneno haya na Martin Luther King Jr.wapo mbumbumbu wanainua simu zao kwa hasira ili wanitukane,maana nachoma moto myoyo yao iliyojaa uovu na hasira za maasi na maangamizi.
 Haidhuru! Mimi siyo ‘coward’ mwoga na Martin Luther King Jr, ni shujaa kwa watu wake hata leo, anasema Wanegro wasingejiwekea heshima kwa kuuza damu za watoto wao vitani.Alisema amani ni kutunza mustakabali wa taifa na vita ni kuweka rehani hatma ya watu wako kwa mtutu wa bunduki.
Alihimiza watu kukabiliana na uovu bila vita na machafuko.Machafuko huleta machafuko na siyo mafanikio.
Alisema, ‘Jino kwa Jino’ ama ‘Jicho kwa Jicho’ hatimaye hulifanya taifa zima kuwa na watu vibogoyo na wenye chongo-hawana meno na  hawana macho! Fikiri kwa makini, hawana meno na hawana macho-vipofu,hawana akili wala umakini kwa utekelezaji wa mambo yao. Vilema.
Martin Luther King Jr. alikariri maneno ya Yesu kwa Mtume Paulo(Yohana 18:10,11) Yesu alimwonya Petro arejeshe upanga wake alani mwake siku Petro alipomkata sikio adui yao aitwaye Malko; Upendo hushinda vita na dhuluma,amini usiamini.
 Tuichunguze hii “Concept” ya Matrin Luther King Junior.ya Nonviolent resistance.Imeleta nini kwa Wanegro ama watu wesi wa Marekani siku hizi?
Avis A. Jones-DeWeever(PhD) ni Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Taifa la Wanawake Weusi(Wanegro)wa Marekani.
Agosti 16 TULIKUWA NAYE katika press conference, Jijini Mwanza. Ni msichana mdogo,msomi aliyekariri maneno ya Martin Luther King Junior,kwamba kila mtu anapaswa kuheshimiwa,kuthaminiwa (valued, validated and respected)na kila mtu napaswa kuishi kwa amani(to live a life free of violence), sasa ukikosa kuthaminiwa ukafanya ghasia,hicho kipande cha kuishi salama umekipata?
Dk.DeWeever, alikumbuka zama za harakati za Weusi wa Marekani kupigania haki zao kwa zaidi ya miongo minne(miaka 40) tangu ilipopitishwa sheria ya HAKI ZA RAIA(Civil Rights Act)ya mwaka 1964. Hatimaye Januari 20 mwaka 2008 Mtu Mweusi,Barack Obama aliapishwa kuwa Rais wa Marekani.
Dk. Martin Luther King Jr. aliuliwa na Pentagon mwaka 1968, ndoto yake ilitimia kwa amani baada ya miaka 40 kamili.
 Vita haviwezi kuwa suluhisho la matatizo ya watu.na ghasia na machafuko siyo njia muafaka kuendea kwenye uhuru dhidi ya dhuluma na ufisadi. Kupigana vita dhidi ya mafisadi na ufisadi ni sawa na kukimbia mbio kutoka kwa Shetani ili kutafuta hifadhi ya ukimbizi kwa Ibilisi,majini yenye kiu ya damu,mapepo wachafu na Lucifer!!
 Mungu ibariki Afrika,Mungu Ibariki Tanzania!
 congesdaima@yahoo.com
0713 324 074










No comments:

Post a Comment