Tuesday, May 29, 2012

MAGAIDI HATARINI KUVAMIA ZIWA VICTORIA

Mwangwi wa A-Shabaab Nairobi, watikisa wasafiri Ziwa Victoria

          *Mabadiliko ya Tabianchi yatishia meli kuparamia miamba na kuzama
        Na Conges Mramba, Mwanza
   MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari(TPA), imewapandisha kizimbani wamiliki wa meli binafsi, kwani wanazuia Mamlaka hiyo kusimamia usalama wa abiria na mizigo, hata wakati huu wa kitisho cha magaidi wa Al-Shabaab,Afrika Mashariki.
 Mkuu wa Bandari(Port Master)Mwanza, John Mutalemwa, katika mahojiano maalum na gazeti hili juzi, alisema wamiliki hao wa Bandari binafsi wanashindana na Sheria Na. 17(Tanzania Port Act) ya mwaka 2004.
Sheria hiyo inaipa TPA  nguvu ya kusimamia bandari zote, zikiwemo za watu binafsi,ili kukagua usalama wa abiria na mizigo,kabla na baada ya safari.
 “Sheria inatupa Mamlaka ya kusimamia bandari zote zikiwemo  bubu, tukague na kujua mizigo kiasi gani inasafirishwa; tunatakiwa kutazama abiria ikiwa wanalingana na uwezo wa meli au boti,kulinganisha na uwezo wa  chombo chenyewe, halafu tunatoa, “Port Clearance” kabla ya meli kuanza safari”, Mutalemwa alisema.
Kwa mujibu wa Mutalemwa, vipo vyombo vya usafiri majini,huchukua abiria na mizigo kuoita uwezo. Hii ni kazi ya TPA kufanya ukaguzi makini,ili kuondokana na Ajali Ziwa Victoria.
 “Bandari ni mpaka wa nchi. Lazima tusimamie hali ya usalama, meli inaweza kuleta Al-Qaeda ama Al-Shabaab, nap engine inaweza kuingiza nchini silaha kutoka nchi za vita na migogoro. Eti wanakataa tusiwasimamie…tumewafungulia kesi mahakamani”,Mutalemwa ameliambia gazeti hili katika mahojiano Maalum ofisini kwake juzi.
 Meli za mizigo za Jijini Mwanza, hufanya safari zake hadi Port Bell, Uganda,na Kisumu nchini Kenya, ambako sasa magaidi wa Al-Shabaab wanasaidia kuzimu kupanua kinywa chake.
 Aidha, Mkuu huyo wa Bandari Mwanza amesema nchi za Maziwa Makuu kama Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, na Burundi hazina amani, na Kenya hamkani si shwari,kufuatia kitisho cha Al-Shabaab, wanaopinga majeshi ya nchi hiyo kuingia Somalia kuwafulusha magaidi hao.
Kufuatia hali tete ya usalama nchi jirani, Mutalemwa amesema lazima Mamlaka yake kuwa macho na usalama wa abiria na mali zao dhidi ya hujuma za magaidi, wanaoweza kupata upenyo wakaingiza silaha nchini kupitia Ziwa Victoria.
  Mamlaka ya Bandari humiliki bandari za Mwanza Kaskazini na Kusini,Nansio Ukerewe,Kemondo Bay    na Musoma.
Vituo vingine vidogo vinavyomilikiwa na TPA ni Maisome,Nkome,Bukondo,Kahunda,Miharaba,Kome,Buchosa,Solima,Karumo,Chato na Nyamirembe(Kagera) na Kinesi mkoani Mara.
 Bandari ya Mwanza ni kiungo muhimu kwa nchi za Maziwa  Makuu,hususan Uganda na Kenya,na huchangia kwa kiwango kikubwa kukua kwa shughuli za uchumi,hata katika nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki(EAC).
 Ripoti ya Malka hii iliyotolewa kwa Kamati ya Bunge ya Miundombinu(nakala tunayo), inasema bandari ya Mwanza ingeweza kusafirisha abiria milioni moja kwa mwaka.
 Ingeweza kusafirisha tani mamilioni za  moja za mizigo,kama Reli ya Kati ingekuwa inafanya kazi kwa ufanisi. Hili ni eneo muhimu kwa ukuaji wa uchumi wan chi,lakini kinyume chake ni hasara kila upande.
 “Huduma hafifu za Reli zimesababisha shehena ya kahawa kutoka Uganda na hata Bukoba,kubadili njia(route) na kupitia Bandari ya Mombasa,Kenya “, Ripoti hii inasema.
 Kufuatia huduma duni za Shirika la Reli, Bandari za Mwanza ziko taaban,kwa sababu ya kupungukiwa mapato, zinaendeshwa bila faida.
 Kulingana na Ripoti hii kwa Kamati ya Bunge ya Miundombinu,katika kipindi cha miaka mitano,kuanzia 2006/2007 hadi 2010/2011, mizigo imepungua katika Bandari za Mwanza kutoka tani 480,568 hadi 248,860 mwaka 2011.
Utendaji mbovu wa lililokuwa Shirika la Reli(TRL) ulisababisha treni iliyokuwa ikisafirisha abiria na mizigo kati ya Mwanza na Bandari ya Dar es salaam kusimamishwa.Hali hii husababishwa abiria na mizigo kubadili njia na kukosesha mapato bandari za Mwanza.
 Wafanyabiashara wa Uganda wanasafirisha bidhaa zao kupitia bandari ya Mombasa,nchini Kenya.Shehena ya kahawa kutoka Uganda iliyokuwa ikipitia bandari za Mwanza, inapitia Mombasa na hivyo kupunguza kiwango cha mizigo kutoka tani 250,000 mwaka 2007 hadi tani 100,000 mwaka 2009/2010.
 Kufuatia madudu ya TRL, hata abiria wamepungua katika bandari za Mwanza kutoka abiria 891,634 mwaka 2007 hadi abiria 593,342.Huu ni upungufu wa asilimia 6.3 unaoikosesha nchi mapato na fursa za ajira kwa watu wake.
 Ripoti hiyo ya TPA, imebaini kwamba, wasafiri wa vyombo vya majini Ziwa Victoria wamepungua kufuatia ushindani uliopo wa barabara,hususan baada ya mtandao wa barabara kukamika ujenzi kwa kiwango cha lami.
 Kati ya Mwanza na Bukoba kuna usafiri wa ndege ambao huchangia pia abiria wasisafiri kwa meli.
Kufuatia hali hiyo,ripoti hiyo imebaini kuwa Kampuni ya Huduma za Meli,Marine Services Company(MSC) iko hatarini kufilisika,kufuatia meli zake kuharibika mara kwa mara,kitu kinachodaiwa na baadhi ya abiria kuwa ni hujuma za baadhi ya wafanyakazo wa MSC ili kuwanufaisha wenye meli binafsi.
  Kaimu Meneja Mkuu wa MSC, Projest Kaija, ameliambia Mwanahalisi kwamba madai hayo hayana ukweli, kwa kuwa kuhujumu kampuni unayofanyia kazi maana yake ni kuhujumu mshahara na mapato yako.
“Je, unahujumu Kampuni namna hiyo ili kampuni ikifa wewe utoe wapi mshahara?’ Kaija alihoji.
 Siku za karibuni MSC imewaondoa viongozi wa Kampuni hiyo na kuwaweka wapya ili kuboresha ufanisi na kupunguza nakisi.
 Kwa kipindi cha miaka mitano, idadi ya meli zilizohudumiwa na Bandari za Mwanza, imepungua kutoka 2,684 hadi meli 1,900 mwaka jana.
Bandari ya Mwanza pia huendeshwa kwa hasara ya mamilioni ya shilingi kila mwaka,nakisi ni takriban shilingi bilioni 4.5
Mabadiliko ya Tabianchi na Ongezeko la Joto Duniani,pia hutishia USALAMA wa usafiri Ziwani Victoria.
Kwa kipindi cha kati ya mwaka 1998 hadi 2006,maji ya Ziwa Victoria yamepungua kutoka mita 1,141.24 juu ya usawa wa bahari hadi mita 1,139.20. Upungufu ni wastani wa mita 2.04.
Kulingana na Ripoti hiyo, meli nyingi zimekuwa zikishindwa kufungwa katika bandari za Mwanza na Nansio,Ukerewe. Kupungua kwa kina cha maji ya Ziwa hili pia huweza kusababisha kuzuka kwa miamba ambayo huhatarisha usalama wa meli na boti na usalama wa abiria,hasa wanaposafiri nyakati za usiku.
Meli zinapoparamia miamba hutoboka na kujaa maji,ama kuwa katika hatari ya kuzama.
 Ziwa Victoria ni chanzo cha Mto Nile, ambao huanzia katika Maporomoko ya Owen,Uganda; maji husafiri umbali wa zaidi ya kilomita 6,900 hadi Misri. Mvua za masika zinaponyesha Afrika ya Mashariki hubeba rutuba mezi ya Aprili na Mei na rutuba hiyo hufika Misri kati ya Agosti na Septemba na kuwawezesha Wamisri kupata rutuba jangwani.
 Mto Nile ni mungu wa Wamisri. Miungu ya Misri ina ‘mama’ yao Ziwa Victoria. Ni kwa sababu hii, mwaka 1929 na 1957 Misri walitiliana saini mkataba na Wakiloni wa Kiingereza kuzuia matumizi ya maji ya Ziwa Victoria kwa shughuli za kilimo na hata vyanzo vya umeme kama kilichopo Jinja.
 Aidha,kupungua kwa kina cha maji ya Ziwa hili hufanya meli kutia nanga katika maji ya kina kirefu,na huku ni kuhatarisha maisha ya abiria,hasa katika maeneo ya visiwa.
 Mkuu wa Bandari ya Mwanza, John Mutalemwa anasema Mamlaka yake imelazimika kuchimba mchanga katika bandari za Mwanza ili kuongeza kina cha futi tatu ili kuwezesha meli kufunga gatini.
 Mradi kama huu unafanyiwa upembuzi yakinifu katika bandari ya Nansio,Ukerewe,lengo likiwa kujenga gati imara na salama.
Mpango wa serikali wa kuunganisha Reli kutoka Tanga hadi Musoma kupitia Arusha, utaweza kurejesha wingi wa abiria na mizigo katika Bandari za Mwanza, au abiria na mizigo ya Uganda,Rwanda,Burundi na Congo wanaweza kutozifikia kabisa bandari za Mwanza,na hivyo kuleta kifo cha mende kwa TPA na Meli za MSC.
Ziwa Victoria ni fursa muhimu kwa Tanzania katika Soko la Pamoja la EAC,lakini fursa hii inaachwa kwa wageni kupitia hujuma na ufisadi unaofanywa na maofisa wa mashirika ya umma kama TRL na MSC.
  www.congesmrambatoday.blogspot.com
    0786 324 074
 
  
 
 

No comments:

Post a Comment